Friday, June 17, 2022

RAS Mwaluko azindua wiki ya utumishi wa umma ki Mkoa, ahimiza viongozi kutimiza wajibu wao na kutoa huduma stahiki kwa mujibu wa sheria katika kuwahudumia Wananchi.

VIONGOZI wa Taasisi za Umma na binafsi mkoani Singida, wamehimizwa kuhakikisha wanajenga mazingira rafiki baina yao na watumishi wanaowaongoza ili kuongeza tija na uwezo wa kutoa huduma mbalimbali zitakazo kidhi mahitaji ya wananchi.

Wito huo umetolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Singida, Dorothy Mwaluko wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa Wiki ya Utumishi wa Umma mkoani Singida uliyofanyika katika ukumbi wa mikutano ofisi ya Mkuu wa mkoa huo Juni 16, 2022.

Amefafanua kwamba wiki ya Utumishi wa umma inalenga kuhamasisha na kuwakumbusha watumishi wa sekta ya umma na binafsi kujua wajibu wao katika kuwahudumia wananchi pamoja na kutambua miiko mila na desturia za utumishi wa umma ambazo zitasaidia kuongoza mahusiano mazuri katika kutekeleza majukumu ya kazi.

“Ili wananchi waweze kuhudumiwa ipasavyo kiongozi wa Taasisi ni lazima awe na mahusiano mazuri na watumishi anaowaongoza. Pia awe na utamaduni wa kuwatembelea watumishi wa chini yake na kujua changamoto zinazowakabili. Changamoto ambazo zipo kwenye uwezo wao wazitatue mapema iwezekanavyo”. Amesisitiza Mwaluko.

Amewasisitiza kutoa huduma kwa wananchi bila upendeleo au ubaguzi wowote na pale wanapokutana na changamoto ambazo zitakuwa juu ya uwezo wao waziwakilishe kwenye mamlaka husika ili ziweze kutafutiwa majibu.

“Wapo baadhi ya viongozi wa taasisi za umma au binafsi hawapo karibu na watumishi wa chini yao. Mtumishi akifanya kakosa kadogo kiongozi badala ya kusaidia kutatua anatishwa na kuambiwa atachukulia hatua kali dhidi ya mtumishi huyo. Tabia hii haijengi na haivumiliki kabisa”. amesema RAS Mwaluko.

Mwaluko amesema ni kweli tunapashwa kusimamia sheria kanuni na taratibu lakini wakati mwingine busara zinatakiwa zitumike hasa ukizingatia  binadamu ni mtu wa makosa.

Aidha, ameonya viongozi wengi wa taasisi za umma na binafsi ambao hawajishughulishi na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi walio chini yao kitendo hicho kinachochea watumishi hao kukimbilia ofisi ya Katibu Tawala Mkoa ambayo imegeuka kuwa kama kliniki.

“Tarehe 23 mwezi wa Nane Sensa tujiandae kuhesabiwa na tukawahimize wananchi wanaokuja kupata huduma kwetu ili waweze kutambua hiyo tarehe kwa ajili ya SENSA ya mwaka huu”. Amesisitiza Dorothy Mwaluko

Kwa upande wake Katibu Chama cha Walimu Mkoa wa Singida, Mwalimu Suzan Shesha ametumia nafasi hiyo kumshukru na kumpongeza Katibu Tawala Mkoa huo Dorothy Mwaluko kwa kubuni na kuanzisha wiki ya utumishi wa umma ambayo itasaidia katika kubadilishana uzoefu na kuongeza hali ya utendaji katika kuwahudumia wananchi.

“Kukutanisha viongozi wa taasisi za umma na binafsi mama yetu Dorothy Mwaluko ameona mbali sana. Sisi viongozi tumepata nafasi ya kutoa changamoto zinazotukabili na zimepatiwa majibu wakati huo huo. Ili kumuunga mkono Katibu Tawala wetu tunaenda kuhakikisha walimu wanawajibika ipasavyo”. Amesema Suzan Shesha

Aidha, Suzan ametumia fursa hiyo kumshukru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kwa mambo mengi mazuri anayowatendea watumishi wakiwemo walimu katika kutatua changamoto mbalimbali pamoja na ile sugu ya kupandishwa madaraja.

Naye, Katibu Chama cha walimu Wilaya ya Mkalama, Amani Msange amesema yale yote aliyoagiza Katibu Tawala Mkoa wanaenda kuyafanyia kazi ikiwemo kutembelea watumishi  na kujua changamoto zinazowakabili na kuzipatia ufumbuzi wa kudumu.


Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dorothy Mwaluko akizungumza na Viongozi wa Taasisi za Umma na Binafsi pamoja na Vyama vya Wafanyakazi mkoa wa Singida katika hafla ya uzinduzi wa wiki ya Utumishi wa Umma iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mkuu wa Mkoa huo tarehe 16 Juni, 2022


Viongozi wa Taasisi za Umma na Binafsi pamoja na Vyama vya Wafanyakazi waliopo mkoani Singida wakizungumza na waandishi wa habari wakati wa mahojiano mara baada ya Uzinduzi wa wiki ya Utumishi wa Umma uliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mkuu wa Mkoa huo tarehe 16 Juni, 2022

No comments:

Post a Comment