Thursday, September 09, 2021

“Serikali itaendelea kuwaunga mkono wawekezaji wazawa”- RC Mahenge.

 

Serikali mkoani Singida imesema itaendelea kuwasimamia na kuwaunga mkono wawekezaji wadogo wa ndani ambao wamewekeza katika sekta tofauti mkoani humo kwa sababu wamekuwa na mchango mkubwa katika ujenzi wa taifa na kuongeza ajira kwa watanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Singinda Dkt. Binilith Mahenge ametoa kauli hiyo leo alipotembelea kiwanda cha maziwa cha muwekezaji mdogo kinachofahamika kwa jina la  TAISH Farm kilichopo katika kijiji cha Mtipa mtaa wa mwembe mmoja katika manispaa ya Singida.

Dkt. Mahenge amebainisha kwamba Serikali itaendelea kutoa mazingira wezeshi  kwa wawekezaji ikiwa ni pamoja na kutatua changamoto zinazowakabili .

Aidha amempongeza mkurungezi wa kiwanda hicho Bw. Hassani Tati kwa kusaidia upatikanaji wa soko la maziwa kutoka kwa wafugaji wadogo ambapo hununua lita zaidi ya 70.

Hata hivyo kiwanda hicho kimekuwa kikizalisha ajira kwa watanzania kupitia mnyororo wa thamani ambapo kiwanda kimeajiri watumishi na wengine kupata ajira katika maduka ya kuuzia maziwa hayo. Alisistiza RC.

Akijibu changamoto za ubovu wa barabara, ukosefu wa umeme zilizotajwa na mkurugenzi wa kiwanda hicho, Mkuu wa Mkoa amewaagiza TANROAD na TARURA  kupeleka ofisini kwake  mpago wa utengenezaji wa barabara hiyo inayoingia kiwandani hapo ili washauriane na kuanza utengenezaji mara moja.

Aidha amewataka shirika la umeme TANESCO  kuhakikisha ndani ya muda mfupi wanafikisha umeme katika eneo hilo la kiwanda ikiwa ni pamoja na vijiji vingine 12  vilivyo ndani ya manispaa ya Singida ili kurahisisha uwekezaji na uboreshwaji wa kiwanda hicho.

Amesema zoezi la upelekaji umeme katika maeneo hayo anaamini litakuwa rahisi kwa kuwa shirika la umeme TANESCO wamepewa Zaidi ya shilingi bilioni tatu (3) ili kusambaza  umeme vijijini  alibainisha Dkt. Mahenge.

Mkuu wa Mkoa amemshauri mwekezaji huyo  kuchukua mkopo benk ili aweze kununua mashine za kisasa kwa ajili ya uongezaji wa thamani ya maziwa  kwa kuwa Serikali itatatua changamoto za barabara pamoja na upatikanaji wa umeme wa uhakika.

Bado una nafasi ya kuongeza uwekezaji na kufanya vizuri zaidi hivyo nakushauri ufungue vituo vidogo vya kukusanyia maziwa  ambapo utakuwa unapima ubora hukohuko, hii itamsaidia mfugaji kutotembea mwendo mrefu na maziwa  yataendelea kuwa salama zaidi”. Alimalizia Mkuu wa Mkoa.

Awali Mkurugenzi wa kiwanda Bwana Hassani Tati akimkaribisha Mkuu wa Mkoa amesema kiwanda hicho kwa muda wa miaka mitano kimekuwa kikitengeneza bidha mbalimbali za maziwa zikiwemo mtindi, maziwa fresh na  yogati zenye ladha tofauti.

Amesema maziwa hayo yananunuliwa kwa wafugaji wa Singida na yanauzwa Manyoni, Ikungi, Singida,  Mkalama, Shelui, Igunga, Ikungi na Dodoma

Aidha Bwana Hassani amebainisha kwamba pamoja na changamoto ambazo Serikali imekiri kuzitatua lakini bado kuna changamoto ya upatikanaji wa vifungashio vya bidhaa hiyo ambapo wanalazimika kuviagiza nje ya nchi.

Mwisho aliomba Serikali kutafuta wawekezaji wengine wa vifungashio ili kuachana na uagizaji wa bidhaaa hiyo nje ya nchi.

Mwisho

No comments:

Post a Comment