Tuesday, April 26, 2022

Maadhimisho ya 58 ya Muungano Singida Yatumika Kuwafunda Vijana

  
Vijana mkoani Singida wametakiwa kujiamini, kuonesha na kuvitumia vipaji walivyonavyo katika kuleta ubunifu na ugunduzi wa mambo kwa kuwa wengi wana vipaji  lakini hawajavitambua.

Akiongea katika Kongamano la maadhimisho ya 58 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha uhasibu (NlT) uliyopo mkoani hapo Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Gerry Muro amewataka vijana kuhakikisha wanatumia akili zaidi kuliko elimu katika kutambua vipaji walivyonavyo na kuchukua hatua.

Akieleza umuhimu wa vijana kutumia akili zaidi kuliko elimu DC Muro amesema kwamba duniani wagunduzi wakubwa hawakutumia elimu lakini walitumia akili na wakafika mbali hivyo kuwataka wajitume na waweze kutumia vipaji vyao kama njia ya kupitisha elimu wanazopata.

Aidha DC Muro amebainisha kwamba kijana anayemaliza chuo na kukaa mtaani akisubiri Serikali itoe ajira ni matokeo mabaya ya matumizi ya vipaji kwa kuwa kila mmoja amepewa kipaji chake.

Amewataka vijana kujiunga katika vikundi na kuvisajili ili waweze kupata mikopo kupitia asilimia Nne katika Halmashauri zao huku akiwakumbusha Maafisa Maendeleo ya Jamii kuendelea kutoa msaada wa mawazo kwa vijana wenye vikundi.

DC Muro ameendelea kusema kwamba huenda matumizi mabaya ya simu janja ndio chanzo cha vijana kushindwa kufikiria vizuri namna ya kutatua changamoto zinazowakabili ikiwemo ugunduzi wa vipaji vyao na namna ya kupata mitaji na utajiri kwa ujumla.

Amewataka vijana kutumia Kongamano kuzitumia fursa ambazo zimekuwa zikioneshwa katika mada mbalimbali zilizowasilishwa, na kila mwenye kipaji kuanza kuzitumia.

Kwa upande wake Afisa Vijana Mmoa wa Singida na mratibu wa Kongamano hilo Fredrick Ndahani amesema lengo la Kongamano hilo ni kuonesha fursa za kiuchumi ambazo zimezunguka Mkoa wa Singida ili waweze kuzitumia na kujikwamua katika maisha yao ya kila siku.

Aidha akieleza jitihada za Serikali katika Mkoa wa Singida zakuwainua vijana amesema katika kipindi cha mwaka 2021/2022 Mkoa umetoa jumla ya Tsh. Milioni 601.4 ikiwa ni mikopo iliyotolewa katika vikundi 133.

Amebainisha kwamba jumla ya ekari 23418 zimetengwa kwa ajili ya vijana ili kufanya shughuli za uwekezaji na michezo katika Wilaya ya Manyoni Ikungi Singida na Itigi.

Afisa vijana huyo wa Mkoa akawataka vijana kuacha kutumika katika matukio ya uvunjifu wa Amani na kujihusisha na mambo ambayo yatawajengea uaminifu mkubwa.

No comments:

Post a Comment