Tuesday, January 15, 2019

RC SINGIDA, AZIAGIZA OFISI ZA WATENDAJI KATA KUWA NA DAWATI LA KUPOKEA TAARIFA ZA CHANGAMOTO, SEKTA YA KILIMO


MKUU wa mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi, ameziagiza ofisi zote za halmashauri za wilaya mkoani Singida kuanzia sasa, ofisi za watendaji Kata zitakuwa vituo vya kupokea taarifa za changamoto mbalimbali zinazohusu sekta ya kilimo. 

Dkt. Nchimbi, ametoa agizo hilo hivi karibuni wakati akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida,  zilizotolewa na shirika la Faida MaLi la jijini Arusha lenye tawi lake mkoani Singida.

Amesema lengo la kuanzisha vituo hivyo, ni kuharakisha kuzitafutia ufumbuzi wa changamoto hizo kabla hazijaanza kuleta madhara makubwa.

Akifafanua zaidi, mkuu wa mkoa huyo ameeleza, pindi ofisi hizo zitakapokuwa zikipokea taarifa za changamoto mbalimbali zinazokabili sekta ya kilimo kwenye maeneo mbalimbali, ni budi kuziwahisha kwenye mamlaka husika ili ziweze kupatiwa ufumbuzi wa kudumu mapema. 

“Serikali ya awamu ya tano imeweka lengo la Tanzania kuwa ya viwanda na uchumi wa kati. Hatuwezi kufikia lengo hilo endapo hatutaweka mkazo mkubwa kwenye sekta ya kilimo”,
“Kuanzia sasa, nawataka Maafisa kilimo na ugavi, wahamishie ofisi zao mashambani kwa wakulima,  wasisubiri wakulima wawafuate, wenyewe ndio wawafuate wakulima huko mashambani”. Amesema Dkt. Nchimbi. 

Aidha, Dkt. Nchimbi amesisitiza kuwa, hataki kusikia afisa kilimo au afisa ugani ameshindwa kwenda shambani kwa wakulima kutokana na mvua kunyesha. 

“Utawasikia wataalam hawa wa kilimo wakiombea mvua inyeshe kidogo kisha ikatike. Hakuna cha mvua kukatika…, mvua itawakatikia hukohuko mashambani. Mvua ni neema na ni baraka kutoka kwa Mungu. Naomba mvua isikimbiwe na wala isisingiziwe”, Dkt. Nchimbi. 

Amesisitiza kuwa, Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli amehimiza viongozi na watendaji wajiamini katika kutatua kero za wananchi, na wananchi hao wafuatwe huko huko waliko. 

Aidha, Mkuu wa mkoa huyo ameahidi Serikali yake ya mkoa wa Singida itaendelea kushirikiana na shirika la Faida MaLi, MIVARF, ByTrade (T) Ltd, SDC na TADE katika kusaidia upatikanaji wa mbegu bora.

Hata hivyo, amemuagiza Afisa Kilimo wa mkoa kushirikiana na wasaidizi wake kuandaa kalenda ya kilimo cha mazao mbalimbali na kuzisambaza kwenye taasisi zikiwemo za madhehebu ya dini, akieleza kuwa, kazi ya kilimo ina Baraka kutoka kwa Mungu.

“Kilimo ni kazi ambayo Mungu ameibariki, na kila mwaka kilimo kinakuwa na nafasi nyingi za ajira. Mungu amekuwa akitoa Baraka zake kwenye kilimo kwa kukipa mvua za kutosha kama ambazo zinanyesha msimu huu”.

“Kwa hiyo, viongozi wa dini wakipata kalenda ya kilimo cha mazao mbalimbali, watatenga muda wa kuwakumbusha waumini wao umuhimu wa kazi ya kilimo. Nina uhakika wakulima waumini watazingatia muda stahiki wa kila zao kwa ajili ya kupanda mbegu bora. Kwa njia hii kilimo kitakuwa na tija zaidi na kitaharakisha kufikia uchumi wa kati” Dkt. Nchimbi. 

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa shirika la Faida MaLi, Bw. Tom Silayo, amesema mbegu ya alizeti ya aina ya Hysun 33, ilijaribiwa mwaka jana na kutoa magunia 18 ya alizeti ghafi kwa ekari moja (1) ikilinganishwa na gunia nne (4) kama ilivyozoeleka.

“Msimu huu tumehamasisha wakulima wapatao 20,460 kutumia mbegu hii ya Hysun 33. Tunachukua na tumeorodhesha majina na namba zao za simu. Wajibu wetu mwingine ni kuhakikisha tunakuza masoko endelevu. Lengo likiwa ni wakulima waendelee kupata faida zaidi ili mwisho wa siku waishi maisha yaliyo bora”. Amesema Silayo.

Naye, Mkulima mdogo Bi. Amina Dafi, pamoja na kulishukuru shirika la Faida MaLi amesema, kuanzia msimu huu wataondokana na matumizi ya mbegu za mazoea (mbegu hasara), na kutumia mbegu bora walizokopeshwa ili waweze kupata mavuno mengi yatakayosaidia kuinua uchumi wao.

Zao la alizeti ni malighafi katika viwanda 144 vya kukamulia mafuta mkoani hapa. Viwanda hivyo vinahitaji tani 482,500 za alizeti ili viweze kufanya kazi kwa kipindi cha mwaka mzima.

Kauli mbiu ya mwaka huu ya kilimo cha alizeti inasema, 
“ALIZETI SINGIDA - BADILI GIA, TUMIA MBEGU BORA”.
 “kauli mbiu hii naomba iwe ni wimbo wa kila siku kwa wakulima mkoani Singida”. Dkt. Nchimbi.

MATUKIO KATIKA PICHA  

 Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi kushoto akisalimiana na Katibu Tawala wa wilaya ya Singida DC Bw. Wilson Shimo mara baada ya kuwasili kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.
 Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi kushoto akisalimiana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Singida DC, Bw. Rashidi Mandoa mara baada ya kuwasili kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.

 Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi kushoto akisalimiana na Mkurugenzi wa shirika la Faida MaLi, Bw. Tom Silayo, mara baada ya kuwasili kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.

 Mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita zilizokopeshwa kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.

 Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Singida DC, Bw. Rashidi Mandoa akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.

 Mkurugenzi wa shirika la Faida MaLi, Bw. Tom Silayo akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.

  Bw. David Vallence kutoka Kampuni ya ByTrade ambao ni wasambazaji wa mbegu Hysun 33 (Chotara), akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida.

 Mkuu wa wilaya ya Singida DC, Mhandisi Paskasi Muragili akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mkopo wa mbegu bora za alizeti aina ya Hysun 33, tani sita kwa wakulima wadogo Tarafa ya Mtinko halmashauri ya wilaya ya Singida..


IMETOLEWA NA;
KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO
OFISI YA MKUU WA MKOA
SINGIDA

No comments:

Post a Comment