Monday, February 16, 2015

WATUMISHI WA SERIKALI KUU MKOANI SINGIDA WAOMBA KUPATIWA "TIN NUMBER".





Picha ya pamoja ya washiriki wa kikao kazi kuhusu Mikopo ya Watumishi wa Serikali kuu, Mgeni rasmi akiwa Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan.

Watumishi wa Serikali Kuu Mkoani Singida wameaswa kuchangamkia fursa ya mikopo kwa watumishi wa Serikali Kuu kupitia mfuko wa "Public Service  Advances Fund- PSAF".

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan ametoa rai hiyo leo asubuhi wakati akifungua kikao kazi kilichoandaliwa na Wizara ya fedha-Hazina ili kuwaelimisha juu ya taratibu za mikopo kwa watumishi wa umma.

Hassan amesema mikopo kwa watumishi wa serikali kuu kupitia mfuko wa PSAF ina riba ndogo na mtumishi anapata kiwango kikubwa cha fedha hivyo kutoa tafsiri halisi ya mkopo huo ya kuwasaidia watumishi hao.
Washiriki wa kikao kazi kuhusu Mikopo ya Watumishi wa Serikali kuu wakifuatilia kikao hicho.

Nao watumishi hao wameiomba Wizara ya fedha kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) iwapatie namba za utambulisho wa mlipa kodi (Taxpayer Identification Number-TIN)  kwakuwa wao hulipa kodi kila mwezi na bila kusita.

Katibu Tawala Msaidizi Utumishi na Rasilimali watu Buhacha Kichinda amesema Wizara hiyo inapaswa kuwatambua watumishi wa serikali kama walipa kodi wazuri  kwakuwa huwa inawatambua walipa kodi wengine kwa kuwapa tunzo kila mwaka. 

Kichinda ameongeza kuwa moja ya masharti ya kupata mikopo ya magari chakavu ni kuwa na 'TIN number' hivyo basi TRA iandae utaratibu wa kuwapatia watumishi wote namba hizo ili namna ya kuonyesha inatambua umuhimu wao kama walipa kodi.
Mhasibu kutoka Idara ya Mhasibu Mkuu Hazina Flora Mahuve akiandika baadhi ya maoni na maswali kutoka kwa washirki wa kikao hicho, katikati ni Mhakiki Mali za Serikali Mkoa wa Singida Ndemfuo Senyaeli Tarimo na wa mwisho ni Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Aziza Mumba.

Mhasibu kutoka Idara ya Mhasibu Mkuu Hazina Flora Mahuve ametoa maelezo juu ya historia ya Mfuko wa PSAF, mtaji wa mfuko huo, huduma na taratibu za mfuko, mafanikio na changamoto za mfuko huo.


Mahuve ameongeza kuwa mfuko wa PSAF unatoa mikopo kwa watumishi wa Serikali kuu peke yake na mikopo hiyo hutolewa kama pesa au mkopo wa gari au pikipiki chakavu ambazo hazifai tena kwa matumizi ya serikali.

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Liana Hassan akiwa na washiriki wa kikao cha Mikopo ya Watumishi wa Serikali kuu mara baada ya kikao hicho.

No comments:

Post a Comment