Saturday, November 09, 2019

"SINGIDA BILA MAGONJWA YASIYO YA KUAMBUKIZA INAWEZEKANA" Dkt. Rehema Nchimbi

Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi (mwenye kofia ya Tanzania) akiongoza wananchi waliojitokeza katika uzinduzi wa kimkoa Mpango wa Taifa wa kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza (NCD) mkoani Singida.

Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Rehema Nchimbi amezindua kampeni ya Mpango wa Taifa wa kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza (NCD) iliyofanyika kimkoa leo Novemba 9, 2019 katika viwanja vya Bomberdia Manispaa ya Singida.

Dkt Nchimbi alisema, swala la afya ni swala la kiusalama, hivyo jamii isiyo na afya bora usalama wake ni mdogo, itakuwa ni jamii ya visasi na kero zisizoisha ndani ya jamii.

Alisema magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanawezekana kuondolewa na kuepukika katika mkoa wa Singida kwa asilimia mia moja kwa njia ya mazoezi, kwani mazoezi ni kinga na ni tiba ya magonjwa huku akiwasihi watumishi wa umma mkoani hapa kula mlo kikamilifu hasa wakati wa asubuhi na mchana ili kulinda na kuimarisha afya itakayoboresha utendaji mzuri wa kazi katika maeneo ya kazi.

Akizungumza kwa msisitizo Dkt. Nchimbi alisema “Magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanazeesha sana, unaonekana mzee kuliko hata umri wako…Tuhakikishe tunajenga Singida yenye sifa ya kuwa na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa asilimia sifuri”.

“Singida yetu ni njema tena ni njema sana… Tuhakikishe tunaijenga Singida yenye sifa ya kuwa na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa asilimia sifuri” Dkt. Nchimbi

Hata hivyo, amemwagiza mganga mkuu wa mkoa pamoja na watoa huduma za afya mkoani hapa kufanya ukaguzi wa mapishi kwenye hoteli zote, migahawa ya baba lishe na mama lishe juu ya mapishi bora, sambamba na kutoa elimu stahiki kuhusu afya ya mlo kamili  ili kudhibiti magonjwa yanayotokana na vyakula vinavyopikwa kwa kutumia mafuta mengi yanayosababisha kuwa na ugonjwa wa shinikizo la damu (presha).

Mkuu huyo wa mkoa amewataka wananchi mkoani hapa kutokula kila chakula kinacholetwa mezani bali kula chakula bora chenye matokeo chanya ndani ya mwili ili kuwa mtu mwenye afya bora ya kimwili na kiakili.

Kwa upande wake Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt. Angelina Lutambi amewasisitiza watumishi wa umma na wananchi wote wa Singida kufanya mazoezi ili kujenga miili yenye afya bora kwa faida ya familia na Taifa kwa ujumla.

“Mpaka vijijini watu wanaumwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza. Hii inaonyesha kuwa kadiri uchumi unavyokuwa vizuri katika jamii zetu ndivyo magonjwa haya yanavyozidi kuongezaka. Hivyo tusipoweka jitihada binafsi tutajikuta tunaugua magonjwa haya” alisema Dkt. Lutambi

Akisisitiza zaidi Dkt. Lutambi amesema moja ya mambo yanayochangia kuongezeka kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza ni mabadiliko ya taratibu za kimaisha zinazohusisha matendo yanayoweza kusababisha ugonjwa.

“Matumizi ya nyenzo za kufanyia kazi au kutofanya mazoezi ya mwili huwafanya watu kulimbikiza nishati lishe mwilini ambazo husababisha ongezeko la uzito wa mwili ambao uchangia kuongeza uwezekano wa kupata magonjwa hayo".  Dkt. Lutambi

Naye, Mganga Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Victorina Ludovick alisema lengo la Serikali kufanya mpango huu ni kutokana na ongezeko kubwa la magonjwa yasiyo ya kuambukiza hasa vifo vinavyotokana na magonjwa haya.

Ameyataja magonjwa hayo ni pamoja na magonjwa ya moyo na mishipa ya damu, mishipa ya fahamu, figo, saratani, kifua sugu, kisukari, meno, macho, magonjwa ya akili na magonjwa ya kurithi kama vile ugonjwa wa selimundu.

Alisema wiki hii itaambatana na kufanya mazoezi ya viungo, huduma mbalimbali za afya zitatolewa ikiwa ni pamoja na upimaji wa shinikizo la damu (presha), huduma za macho na meno, upimaji uzito na urefu ili kuangalia uwiano wa urefu na uzito kama uko sahihi katika mwili.

Dkt. Ludovick ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Singida kushiriki kikamilifu katika mazoezi na huduma zinazoendelea kutolewa katika viwanja hivyo vya bombardier katika wiki hi ili kupata elimu na huduma mbalimbali za kiafya zinazotolewa bila malipo yoyote.

Uzinduzi rasmi wa Mpango huu kitaifa utafanyika Novemba 14, 2019 katika uwanja wa Jamhuri mkoani Dodoma ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (MB) Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pamoja na kuhutubia umma, Mgeni Rasmi atazindua Nembo na Jina la Mpango, atakabidhi vitendea kazi maalum vya Mpango kwa ngazi ya Kituo cha Afya.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt. Angelina Lutambi (wa nne kutoka kulia), Mganga Mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Victorina Ludovick (wa tatu kutoka kulia) wakiwa katika moja ya mazoezi ya viungo ikiwa ni utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza (NCD) iliyofanyika leo Novemba 9, 2019 katika viwanja vya Bomberdia Manispaa ya Singida.

KAULI MBIU: “Tutembee pamoja katika kuzuia na kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza”

MATUKIO MBALIMBALI KATIKA PICHA




 















Habari zaidi tembelea tovuti ya Serikali ya Mkoa: www.singida.go.tz

No comments:

Post a Comment