Tuesday, April 12, 2022

RC Mahenge Aridhishwa na Kasi ya Maendeleo ya Miradi Iramba.

MKUU wa Mkoa wa Singida Dk. Binilith  Mahenge ameridhishwa na kasi ya ujenzi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika Wilaya ya Iramba mkoani  hapa ikihusisha ujenzi wa  vituo vya afya, shule na visima vya maji lengo likiwa ni kusogeza huduma za kijamii kwa wananchi na kuondoa msongamano.

Akiongea leo na viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Iramba Rc Mahenge ametaja miradi inayotekelezwa kwamba ni ujenzi wa shule ya Sekondari Maluga  inayotarajiwa kugharimu kiasi cha Tsh. Milioni 470, ujenzi wa vituo vya Afya vinne (4) vya Tyegelo, Kisiriri, Mwanduigembe na Ndulungu  pamoja na ujezi wa vyumba viwili vya madarasa  katika shule ya Sekondari za Tulya na Kisiriri ambavyo kwa ujumla wake vinagharimu kiasi cha Tsh.  Bilion 1.525 zitokanazo na tozo ya miamala ya simu.

Aidha RC Mahenge akawataka wasimamizi na wahandisi wa miradi mbalimbali wilayani hapo kuiga mifano ya miradi inaotekelezwa na Wakala wa usambazaji wa maji Vijijini na usafi wa mazingira  (RUWASA) ambapo wamekuwa wakisimamia miradi yao  kwa ufanisi na kuhakikisha thamani ya fedha inaonekana.

Katika taarifa yao RUWASA imeonesha kwamba katika Wilaya ya Iramba wana miradi mikubwa mitano (5)  katika vijiji vitano vya Maluga, Zinziligi, Kisiriri, wembere na Kaselya  pamoja na uchimbaji wa visima 24  katika vijiji mbalimbali ambapo miradi yote inagharimu kiasi cha Tsh.Bilion 3.304 na imetekelezwa kwa asilimia 70.

Awali akimkaribisha Mkuu wa Mkoa huyo, DC wa Iramba Suleimani Mwenda alisema Wilaya imepokea jumla ya Tsh.Bilion 1.119 kwa ajili ya Ujenzi wa miradi ya maji katika vijiji vinne huku ikipokea jumla ya Tsh. Milioni 940 kwa ajili ya Ujenzi wa shule mpya za Kata ya Maluga na Ndulungu.

Hata hivyo DC Mwenda akabainisha kwamba Wilaya ya Iramba imepata    fedha  kiasi cha Tsh. Bilioni 1.473 zitokanazo na  ruzuku kutoka Serikali kuu ambapo zinatumika katika Ujenzi wa Kituo cha Afya cha Mtoa na ukamishaji wa madarasa 10 ya shule za msingi.

Aidha fedha hizo zinatumika pia katika Ujenzi wa madarasa Sita katika Shule za Sekondari sita pamoja na ukamilishaji wa vyumba  10 vya Maabara katika Shule za Sekondari tano wilayani hapo aliendelea kusema DC Mwenda.

MATUKIO KATIKA PICHA

                                                                     



Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge akizungumza mara baada ya kujionea hali ya ujenzi wa kituo cha Afya Kisisiri wakati wa ziara yake leo Aprili 12, 2022

Ziara ikiendelea

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Iramba Hussein Sepoko (katikati) akitoa ufafanuzi kuhusu ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za Afya katika Wilaya hiyo wakati wa ziara

Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge akisisitiza jambo wakati wa ziara hiyo


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge akikagua moja ya mradi wa ujenzi wa shule ya Sekonda uliyopo katika kijiji cha Maluga unaoendelea kujengwa wilayani Iramba

Mkuu wa Wilaya ya Iramba Suleimani Mwenda (kulia) akimhakikishia Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge, ukamilishaji wa miradi yote inayoendelea kutekelezwa wilayani humo

Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijiji wilaya ya Iramba Mhandisi Ezra Mwacha akitoa taarifa ya Miradi ya Maji katika Wilaya hiyo wakati wa ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge.

Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Singida Mhandisi Lucas Japhary akizungumza wakati wa ziara hiyo.

Mradi wa Maji katika Kijiji cha Maluga wilayani Iramba

 www.singida.go.tz

No comments:

Post a Comment