Wednesday, August 24, 2022

RC SERUKAMBA AAGIZA UTEKELEZAJI WA KUKATA BIMA YA AFYA YA KILA MWANANCHI KUTEKELEZWA

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Peter Serukamba akizungumza wakati wa kikao cha Menejimenti kwa lengo la kujadili Mpango Mkakati wa kuhakikisha agizo la kila mwananchi anakata bima ya Afya ya CHF iliyoboreshwa kilichofanyika katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa mkoa huo Agosti 24, 2022.

Mkuu wa Mkoa  wa Singida Peter Serukamba ameagiza kuanza kutekelezwa kwa agizo lake la kuhakikisha kila mwananchi Mkoani hapo anakuwa na bima ya Afya ya CHF iliyoboreshwa kama hatua moja wapo ya kupambana na adui maradhi.

Akiongea wakati wa kikao cha Menejimenti kilichofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa ofisi hiyo Serukamba amewataka wataalamu wa Idara ya Afya kuanza mara moja kutambua Kaya zote ambazo zitahusika kwenye ukataji wa Bima ya Afya.

Aidha RC Serukamba amesema wataalamu hao pamoja na utambuzi wa Kaya waendelee kutoa elimu na  uhamasishaji juu ya Bima hiyo kwa wananchi ambapo ameahidi kuzunguka Kata zote 136 za Mkoa wa Singida ili kuhamasisha wananchi na viongozi mbalimbali lengo likiwa ni kupata Bima hiyo.

Lengo la kikao hicho ni kuandaa mkakati wa namna ya kuhakikisha kila mwananchi mkoani humo anapata Bima ya Afya ili waweze kufaidi uwepo wa vituo vya Afya na Zahanati ambazo zimejengwa maeneo mbalimbali Mkoani hapo.

RC Serukamba amesema ili Mkoa uweze kuinuka ki uchumi unahitaji kuwa na watu wenye Afya Bora ambayo itapatikana kwa kila mtu kuwa na Bima ya Afya.

Amesema Mkoa inakadiriwa kuwa na Kaya laki tatu (300,000) na endapo kila mwananchi atachangia Bima ya Afya ya SH.30,000 kwa mwaka Mkoa utapata zaidi ya Bilioni 9 ambapo bajeti ya dawa kwa  mwaka ni kiasi cha Bilioni 8 hivyo hakutakuwa na upungufu wa dawa vifaa tiba na vitenganishi.

Hata hivyo RC Serukamba amesisitiza miradi mbalimbali ya kilimo isimamiwe vizuri na iweze kutumika kuleta matokeo chanya kwa wakulima na wananchi kwa ujumla.

Akitolea mfano Skimu ya Itagata iliyoko Halmashauri ya Itigi Wilayani Manyoni ambayo Serikali imetumia fedha  nyingi kiasi cha Milioni 735 na ilitegemewa kuhudumia wakulima 209 ambapo kwa sasa ina hudumia wakulima wachache na wengine waliendelea kuhodhi maeneo bila kuyatumia.

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Mwl. Dorothy Mwaluko akizungumza wakati wa kikao cha Menejimenti kwa lengo la kujadili Mpango Mkakati wa kuhakikisha agizo la kila mwananchi anakata bima ya Afya ya CHF iliyoboreshwa kilichofanyika katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa mkoa huo Agosti 24, 2022.

No comments:

Post a Comment