Sunday, November 21, 2021

Waratibu wa Miradi Singida Wafundwa

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Bi. Dorothy Mwaluko 

Wasimamizi na waratibu wa miradi mbalimbali ya kijamii Mkoani Singida wametakiwa kuongeza juhudi katika usimamizi kwenye utekelezaji wa miradi hiyo ili iweze kuleta tija kwa jamii husika kama inavyotegemewa.


Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni na Katibu Tawala Mkoa wa Singida Bi. Dorothy Mwaluko alipokuwa anafungua  Kikao kazi cha Mradi wa timiza malengo awamu ya pili kilichofanyika Katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo ambapo amesema wanufaika wa miradi hiyo wanatakiwa kuhitimu na kufikia mwisho ili wengine waweze kupata huduma hiyo.


Amesema kuna miradi tokea imeanzishwa imebaki na wanufaika hao hao mpaka inaisha jambo ambalo halipendezi, inapaswa kuwepo  utaratibu wa wanufaika kuhitimu baada ya muda na kupisha  wengine badala ya kuendelea kuwakumbatia  alibainisha Mwaluko.


Akitole mfano Mradi wa TASAF amebainisha kwamba waliopewa mitaji wanatakiwa kufika wakati wajiendeze wenyewe badala ya kusubiri msaada kutoka Serikalini kila wakati ili kuendeleza  miradi yao kutoa fursa kwa wengine kupatiwa mtaji hiyo.


Aidha  Mwaluko amewataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kuhakikisha miradi  wanajamii wanayoianzisha ni ile waliyopendekeza  wenyewe ili iwe rahisi kuisimamia vizuri  huku akiwataka maafisa hao kuendelea kuwasimamia na kuwashauri katika miradi waliyochagua.


Hata hivyo amezitaka Halmashauri kutumia asilimia kumi za fedha wanazozitenga kwa ajili ya wananwake, vijana na walemavu  kuwakopesha vijana  walioanzisha miradi na kuonekana kupiga hatua.


 RAS huyo akamalizia kwa kutoa wito kwa wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia kuwezesha wenye mahitaji  kupitia miradi mbalimbali kwa kuwa Serikali peke yake haiwezi kufanya kila kitu.


Mratibu wa masuala ya UKIMWI  Mkoani hapo Bw.H.Samiti amesema kwamba Mradi huo ulishamalizika awamu ya kwanza na Sasa wameanza awamu ya pili kwa kuendelea kuwanoa wataalamu mbalimbali ambao watatoa elimu mbalimbali kwa vijana.


Amesema vijana wengi wamenufaika na Mradi huo kwa awamu ya kwanza hivyo wanategemea kuwawezesha vijana wengine kwa kushirikiana na mashirika mbalimbali ili kuwasaidia vijana hao kufikia malengo.


 Eriko Kiwanga ni Mratibu wa Shirika la TACAIDS  anasema Katika Mradi wa  timiza malengo awamu ya kwanza umefanikiwa kwa kiasi kikubwa Katika kuwasaidia vijana walioko ndani na nje ya shule katika kujitambua na kupambana na kuepuka magonjwa ya uzazi na UKIMWI kwa kiasi kikubwa.


Amesema pamoja na mafanikio hayo Mradi umekuwa na changamoto ndogo ya namna ya utoaji wa mitaji ambayo ilikuwa ikitolewa kwa awamu mbili na kusababisha bàadhi ya vijana kushindwa kufanya vizuri kwa kuwa fedha zilikuwa zikija nje ya msimu hasa kwa wale wanaofanya miradi ya Kilimo


Amesema Katika awamu ya pili Shirika limeboresha mambo mengi ikiwepo kutoa elimu kwa Maafisa ugani pamoja na kuleta fedha hizo kwa wakati pamoja na kuongeza usimamizi ili kuleta tija iliyo kusudiwa.


Naye Mariamu Omari Mkazi wa Manispaa ya Singida ni moja ya wanufaika wa Mradi wa Timiza malengo awamu ya kwanza ambaye  pamoja na kushukuru Mradi huo kwa kuweza kubadisha Maisha yake ambapo anajihusisha na saluni ya kike na urembo ameiomba Serikali kuongeza kiwango Cha mitaji kwa kuwa kiasi Cha laki nne kinachotolewa ni kidogo kwa kuanzisha Mradi.

No comments:

Post a Comment