Wednesday, February 27, 2019

RC SINGIDA, ATOA ONYO KWA WATENDAJI WATAKAOWAJIBIKA KUSAJILI VIZAZI KWA WATOTO WENYE UMRI CHINI YA MIAKA MITANO


MKUU wa mkoa wa Singida, Dkt. Rehema Nchimbi, amewaonya watendaji watakaowajibika kusajili vizazi kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano wasithubutu kuleta urasimu wa aina yoyote. 

Dkt. Nchimbi ametoa onyo hilo wakati akizindua semina kwa viongozi wa wilaya na mkoa wa Singida kuhusu mpango wa usajili wa watoto chini ya miaka mitano (Under five birth registration program), uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano ofisi ya mkuu wa mkoa.

Amewatahadharisha wasitangulize mbele masuala ya posho bali watekeleze wajibu wao huo huku wakitarajia thawabu na zawadi kutoka kwa mwenyezi Mungu. 

Amesema usajili huo utasaidia Serikali ya awamu ya Tano kujipanga vema katika kuwahudumia Watanzania kwamadai  Serikali itakuwa na idadi sahihi ya watanzania. 
“Sitaki kabisa kusikia saa za kazi mtendaji hayupo ofisini, ofisi imefungwa, hakuna karatasi au kompyuta imekorofisha. Urasimu wa aina yoyote ni lazima utakula kichwa cha mtendaji” Dkt. Nchimbi.

Aidha, Dkt. Nchimbi amewaomba viongozi wa madhehebu ya dini mbalimbali kutenga muda mfupi kwa ajili ya kuhamasisha waumini wao juu ya mpango wa usajili wa watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano.

“Kusajili watoto sio dhambi, lengo ni zuri tu, nalo ni kujua idadi ya watanzania ili Serikali iweze kupanga namna bora ya kuwahudumia” amesema.

Mkuu huyo wa mkoa, amesema semina hiyo ibadilike na kuwa kikao cha kazi ili iweke mikakati itakayouwezesha mkoa wa Singida kuvuka lengo, na kusajili watoto zaidi. 

Awali kaimu mtendaji mkuu wa wakala wa usajili ufilisi na udhamini (RITA), Emmy Kalomba Hudson, amesema mpango wa usajili wa watoto wa umri wa chini ya miaka mitano unatarajiwa kuanza wakati wowote kuanzia sasa. 

Emmy Kalomba Hudson Amesema, lengo la kuandaa semina hiyo ni kuwapa uelewa wa kina viongozi wote katika ngazi ya mkoa na wilaya, ili waweze kujua kwa kina mambo yote  muhimu yanayohusu mpango huo. 

Akiijengea nguvu hoja yake hiyo, Emmy amesema, usajili  huo ni hatua inayomwezesha mwananchi kutambuliwa kwa kusajiliwa na kupata cheti cha kuzaliwa. Cheti hicho ni kiambatanishi cha kumwezasha mhusika  kupata haki mbalimbali na huduma nyingine nyingi za kijamii.


Akionyesha imani kwamba mkoa wa Singida utafanya vizuri katika kutekeleza mradi huo, kaimu mtendaji huyo, amesema mwaka 2016 mkoa wa Njombe ukiwa chini ya usimamizi wa Dkt. Nchimbi, uliweza kusajili watoto asilimia 99.6 kwa kipindi cha miezi mitatu tu.

MATUKIO KATIKA PICHA

 
 Kaimu Mtendaji Mkuu wa wakala wa usajili ufilisi na udhamini (RITA), Emmy Kalomba Hudson akizungumza.

   






 




 
 


 
 "Cheti cha kuzaliwa ni msingi wa mafanikio yako"

IMETOLEWA NA; 
KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO
OFISI YA MKUU WA MKOA
SINGIDA

No comments:

Post a Comment