Monday, October 10, 2022

Rc Serukamba atoa siku saba kwa watumishi wa Idara ya fedha ya Halmashauri ya Wilaya ya Iramba kuzirejesha Sh.Milioni 365 fedha zilizokusanywa kupitia ushuru na kodi kutoka kwa wananchi.

 

MKUU wa Mkoa wa Singida, Peter Serukamba, ametoa siku saba kwa watumishi wa Idara ya fedha ya Halmashauri ya Wilaya ya Iramba kuzirejesha Sh.Milioni 365 ambazo ni fedha zilizokusanywa na watumishi na mawakala kama ushuru na kodi kutoka kwa wananchi.

Watumishi na mawakala hao walizikusanya fedha hizo badala ya kuzipeleka benki kwenye akaunti za serikali waliamua kuzitafuna ambapo tatizo hilo limekuwa likijitokeza kila mwaka.

Serukamba akizungumza na wakuu wa idara, wahasibu na watendaji wa vijiji na kata leo alisema Halmashauri ya Wilaya ya Iramba ndio inayoongoza kati ya halmashauri saba za Mkoa wa Singida kwa watumishi wake kukusanya fedha na kuzitafuta bila kuzipeleka benki.

"Mumeenda kwenye masoko wananchi wema wamelipa ushuru na kodi lakini mtumishi tuliokupa jukumu la kukusanya fedha baada ya kuzikusanya badala ya kuzipeleka benki unaamua kuziweka mfukon maana yake tumekupa mtaji hili jambo haliwezekani," alisema.

Alisema katika kipindi chake akiwa Mkuu wa Mkoa wa Singida kama kuna mtumishi anadhani hawezi kukusanya fedha za serikali na  kuzipeleka benki au halmashauri basi aache kazi hii haraka.

Serukamba alisema katika ufisadi huu kuna mambo mawili yanajitokeza inawekezekana kuna njama kati ya wakuu wa idara na wakusanyaji ambapo fedha hizo zikikusanywa wanagawana na hivyo serikali kukosa mapato.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda, alisema tatizo hili limekuwa sugu katika wilaya hii ambapo mwaka jana watumishi na mawakala walikuwa wanadaiwa zaidi ya Sh.millioni 200 lakini mwaka huu deni limeongezeka na kufikia zaidi ya Sh.milioni 300.

Mwenda alisema wakuu wa serikali walishafika katika wilaya ya Iramba akiwamo Waziri Mkuu,Kassim Majaliwa ambao waliagiza fedha hizo zilizotafunwa na watumishi zirejeshwe lakini utekelezaji wake umekuwa hafifu.

"Jambo hili limekuwa la muda mrefu, mwaka jana watendaji walikuwa wanadaiwa zaidi ya Sh.milioni 200 pamoja na serikali kuchukua hatua kwa watumishi waliohusika cha kushangaza ufujaji umeongezeka na kufikia Sh.milioni 300 sasa," alisema.

Baada ya maelezo hayo ya Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa alianza kusoma majina ya watumishi na mawakala wanaodaiwa mamilioni hayo ya fedha na kila mmoja kutakiwa kujieleza lini atalipa deni lake.

Hata hivyo, Serukamba alishtuka maelezo ya utetezi yaliyokuwa yanatolewa na wadaiwa na kubaini kuna mchezo mchafu (njama) iliyokuwa imetengenezwa kati ya wadaiwa na watumishi wa idara ya fedha.

Kutokana na hali hiyo, Mkuu wa Mkoa alimua kuwagiza watumishi wa idara ya fedha kuwafuatilia wadaiwa wote na fedha hizo kuzirejesha ndani ya siku saba na kuahidi kufikia katika wilaya hiyo siku ya Jumatatu ya wiki ijayo kuangalia kama fedha hizo zimerejeshwa.

Aisha, alimwagiza Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, Michael Matomora kufuatilia suala hilo ili fedha hizo zirejeshwe ndani ya siku saba.

 


No comments:

Post a Comment