
Mkoa wa Singida unatarajiwa kuanza kunufaika na rasilimali zake adhimu ikiwemo madini yanayopatikana katika hifadhi na mapori tengefu yaliyopo mkoani hapa.
Hayo yamethibitishwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego wakati wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo inayofanywa na Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Singida Wilayani Manyoni kama moja ya kufatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama Tawala.
Mhe.Dendego amesema kwamba kuna taarifa za uwepo wa madini katika mapori ya akiba ya Rungwa,Kizigo na Muhesi ambapo inadaiwa kuwanufaisha watu wachache ambao wamevamia maeneo hayo na kufanya shughuli za uchimbaji madini bila kibali maalumu.
"Maeneo hayo yamekua na madini na vijana wanavamia pasipo mpangilio hivyo tufanye utafiti kubaini maeneo hayo Ili tuombe kibali kwa Mamlaka husika wananchi wetu na vijana wetu waweze kupata leseni Ili wachimbe kwa kufata utaratibu na hii itakuza mapato kwa wananchi wetu lakini pia kwa Halmashauri husika"
Kutokana na hilo ameunda kamati ya wajumbe maalum ya kufanya utafiti wa kina juu ya uwepo wa madini hayo katika mapori hayo sambamba na kutambua mipaka ya eneo hilo.Kamati hiyo inajumuisha Wakuu wa Wilaya ya Manyoni na Iramba,Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni,Afisa Viwanda na Biashara Mkoa wa Singida na wengineo.
Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Singida,Mhe.Martha Mlata akizungumzia suala hilo amesema kuwa Mkoa wa Singida unakwenda kupata neema kubwa ya maendeleo ya kasi kutokana na uwepo wa kibali na leseni ya umiliki wa maeneo hayo adhimu yenye madini hayo kwani baada ya kupata kibali hicho Taasisi,Halmashauri,watu binafsi na wananchi wa Singida kwa ujumla watapata nafasi ya kumiliki vitalu vya uchimbaji madini hivyo kukuza vipato vyao.
Kadhalika ameshauri leseni zilizopo kwa sasa zifutwe kwanza baada ya utafiti ili wanufaika wa kwanza wa madini hayo wawe wananchi wa Singida na Halmashauri zake ambapo zitapewa leseni ya kuajiri wachimbaji wadogo na kuwezesha Halmashauri kukuza mapato sambamba na ajira kwa wachimbaji wadogo.
Awali,Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Dendego amethibitisha kuwa Mhifadhi na Waziri wa Maliasili ma Utalii wameridhia ufanyike utaratibu wa kutambua maeneo hayo yenye madini ili kuombewa kibali ambazo zitawezesha utolewaji wa leseni zitakazowawezesha wachimbaji kufanya shughuli zao.
Upatikanaji wa madini katika maeneo hayo Mkoani Singida unatarajiwa kuwa chachu kubwa ya maendeleo kwani uchumi utakua kwa kasi sambamba na maendeleo ya miji kwani barabara nzuri,sehemu za kulala wageni,hoteli za kisasa ni baadhi ya mabadiliko chanya yanayotarajiwa kutokea.Pia Mkoa wa Singida umebarikiwa kwa madini meupe "gypsum"yanayopatikana maeneo tofauti ikiwemo Halmashauri ya Itigi na Manyoni.