Wednesday, June 11, 2025

WANANCHI WA SINGIDA WALETEWA "UGALI MEZANI"


Posted on: June 11th, 2025

Mkoa wa Singida unatarajiwa kuanza kunufaika na rasilimali zake adhimu ikiwemo madini yanayopatikana katika hifadhi  na mapori tengefu yaliyopo mkoani hapa.

Hayo yamethibitishwa na Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego wakati wa ukaguzi wa miradi ya maendeleo inayofanywa na Kamati ya Siasa ya Mkoa wa Singida Wilayani Manyoni kama moja ya kufatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama Tawala.

Mhe.Dendego amesema kwamba kuna taarifa za uwepo wa madini katika mapori ya akiba ya Rungwa,Kizigo na Muhesi ambapo inadaiwa kuwanufaisha watu wachache ambao wamevamia maeneo hayo na kufanya shughuli za uchimbaji madini bila kibali maalumu.

"Maeneo hayo yamekua na madini na vijana wanavamia pasipo mpangilio hivyo tufanye utafiti kubaini maeneo hayo Ili tuombe kibali kwa Mamlaka husika wananchi wetu na vijana wetu waweze kupata leseni Ili wachimbe kwa kufata utaratibu na hii itakuza mapato kwa wananchi wetu lakini pia kwa Halmashauri husika"

Kutokana na hilo ameunda kamati ya wajumbe maalum ya kufanya utafiti wa kina juu ya uwepo wa madini hayo katika mapori hayo sambamba na kutambua mipaka ya eneo hilo.Kamati hiyo inajumuisha Wakuu wa Wilaya ya Manyoni na Iramba,Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manyoni,Afisa Viwanda na Biashara Mkoa wa Singida na wengineo.

Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Singida,Mhe.Martha Mlata akizungumzia suala hilo amesema kuwa Mkoa wa Singida unakwenda kupata neema kubwa ya maendeleo ya kasi kutokana na uwepo wa kibali na leseni ya umiliki wa maeneo hayo adhimu yenye madini hayo kwani baada ya kupata kibali hicho Taasisi,Halmashauri,watu binafsi na wananchi wa Singida kwa ujumla watapata nafasi ya kumiliki vitalu vya uchimbaji madini hivyo kukuza vipato vyao.

Kadhalika ameshauri leseni zilizopo kwa sasa zifutwe kwanza baada ya utafiti ili wanufaika wa kwanza wa madini hayo wawe wananchi wa Singida na Halmashauri zake ambapo zitapewa leseni ya kuajiri wachimbaji wadogo na kuwezesha Halmashauri kukuza mapato sambamba na ajira kwa wachimbaji wadogo.

Awali,Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Dendego amethibitisha kuwa Mhifadhi na Waziri wa Maliasili ma Utalii wameridhia ufanyike utaratibu wa kutambua maeneo hayo yenye madini ili kuombewa kibali ambazo zitawezesha utolewaji wa leseni zitakazowawezesha wachimbaji kufanya shughuli zao.

Upatikanaji wa madini katika maeneo hayo Mkoani Singida unatarajiwa kuwa chachu kubwa ya maendeleo kwani uchumi utakua kwa kasi sambamba na maendeleo ya miji kwani barabara nzuri,sehemu za kulala wageni,hoteli za kisasa ni baadhi ya mabadiliko chanya yanayotarajiwa kutokea.Pia Mkoa wa Singida umebarikiwa kwa madini meupe "gypsum"yanayopatikana maeneo tofauti ikiwemo Halmashauri ya Itigi na Manyoni.

Saturday, June 07, 2025

"WAUMINI TUTUNZE AMANI NA UTULIVU TULIO NAO":RC DENDEGO

Posted on: June 7th, 2025

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amesisitiza umuhimu wa kutunza amani na utulivu katika Taifa letu,akisisitiza waumini kuendelea kutunza umoja na ushirikiano walio nao kama nyanja muhimu ya kuwaweka pamoja na kufanya shughuli za maendeleo yao binafsi na Taifa kwa ujumla.

Ameyasema hayo leo Juni 7,2025 katika kanisa la Unyankindi Mkoani Singida wakati alipoalikwa kama Mgeni rasmi wa Harambee ya ujenzi wa kanisa hilo  ambapo pia amewahimiza wananchi kutumia jukwaa la Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu vema kwa ajili ya kuchagua viongozi bora watakaowaletea maendeleo na kuitunza amani iliyopo hapa nchini.

“Tunaenda kwenye uchaguzi mwaka huu. Tuendelee kuomba amani. Suala hilo litufikie na liishe salama. Tuwe wamoja – iwe Waislamu, Wakristo, KKKT au dhehebu lolote – tuwe wamoja katika kulinda amani,” amesema Mhe. Dendego


Aidha, Mkuu wa Mkoa amesisitiza kuwa kusaidia kwenye ujenzi wa nyumba za ibada ni sehemu ya maandalizi ya safari ya kiroho ya kila mwanadamu hivyo ni vema kila mmoja kushiriki ili kuwezesha kazi ya Mungu kusonga mbele kadhalika na kumpa kila mmoja baraka.


“Msafiri bora ni yule aliyefunga mizigo yake sawasawa.. na mizigo hiyo ni kama hii ya ujenzi wa kanisa, kusaidia maskini, kuwajali yatima. Haya yote yanatuandalia safari njema ya kesho,” 

Naye Mchungaji Livingstone kutoka nchini Kenya,akizungumza qakati wa harambee hiyo,amewaasa Watanzania kuilinda na kuitunza vizuri amani waliyonayo kwqni ni hazina kubwa kwa nchi ya Tanzania kutokana na utulivu uliopo nchini Tanzania ambao unawapa wananchi nafasi ya kushiriki vema katika shughuli za uzalishaji ambazo  zimekua kichocheo kikubwa cha maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.


“Nimesafiri nchi nyingi sana, lakini amani ya Tanzania ni ya kipekee. Tanzania mna amani sana chini ya uongozi huu. Ithaminini hiyo amani yenu,” amesema.

Kwa upande wake, Mchungaji Dr. David, Askofu Mkuu wa Kanda ya Kati wa Kanisa la Waadventista Wasabato, amemshukuru Mgeni rasmi wa Shughuli hiyo- Mkuu wa Mkoa na waumini wote wa ujumla kwa kukubali kushiriki katika harambee hiyo iliyogusa mioyo yao na kufanikiwa kufikia lengo lililotarajiwa.

Katika harambee hiyo iliyokua na lengo la kukusanya jumla ya Shilingi Milioni mia moja,imefanikisha kupata zaidi ya shilingi milioni mia moja na kuvuka lengo lililopangwa hapo awali huku Mkuu wa Mkoa akichangia kiasi cha Milioni 15.


Monday, June 02, 2025

MRADI WA TACTIC KULETA NEEMA MANISPAA YA SINGIDA

 

Posted on: June 2nd, 2025

Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI Mhe. Zainab Katimba (Mb)  Amewasihi wananchi wa Manispaa ya Singida kutoa ushirikiano kwa Mkandarasi anayetekeleza mradi wa TACTIC pamoja na kutunza miundombinu inayojengwa pale itakapokamilika ili iweze kuwa na tija iliyokusudiwa na kudumu  kwa muda mrefu zaidi, akiziagiza Halmashauri zote zenye miradi ya TACTIC kusimamia vyema uendeshaji wa masoko na Vituo vya Mabasi ili kuzalisha mapato yaliyotarajiwa na Serikali kwa maendeleo ya maeneo yao.

Mhe.Katimba amesema kukamilika kwa utekelezaji wa miradi ya uboreshaji miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) awamu ya pili Kwenye Manispaa ya Singida kutaleta mabadiliko chanya kwenye huduma, manunuzi na mazingira bora ya kufanyia biashara kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wa Mkoa wa Singida.

Ameyasema leo Juni 2,2025 katika hafla ya utiaji saini Miradi ya  Ujenzi wa Soko la Kimataifa la Vitunguu katika viwanja namba 835 na 836, Mtaa wa Misuna, lenye jumla ya mita za mraba 14,465. Jengo la ghorofa mbili, barabara za mzunguko zenye urefu wa mita 700 zitakazojengwa kwa kiwango cha lami,Ujenzi wa Barabara za Mjini Kati na Viwandani, zinazolenga kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na huduma na Ujenzi wa Mtaro wa Maji ya Mvua Mnang’una unaotarajiwa kuzuia mafuriko na kulinda mazingira ya mijini.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego, ametumia jukwaa hilo kueleza dhamira ya Mkoa wa Singida kujiimarisha kiuchumi na kuchangia kwa kiasi kikubwa pato la taifa. 

"Sisi ni majirani wa Makao Makuu ya nchi, Dodoma. Hivyo tumeamua kutumia nafasi yetu ya kijiografia kuwa mkoa wa mfano na kuwa jiji tarajiwa la kanda ya kati," amesema Mhe. Dendego.

Ameongeza kuwa, Mkoa wa Singida umeendelea kuwa mwenyeji mzuri wa wageni na wawekezaji, hasa baada ya kuwa mwenyeji wa Maadhimisho ya Kitaifa ya Mei Mosi, ambapo watu kutoka ndani na nje ya nchi walifika na kuvutiwa na fursa zilizopo akisema kuwa ushirikiano baina ya serikali, sekta binafsi na wananchi ndio nguzo ya mafanikio hayo. 

"Sisi wana Singida tumeamua kupindua meza na kuwa mkoa bora Tanzania. Tuna kila sababu ya kufanikiwa; rasilimali tunazo, nia tunayo, na Mungu ametujalia ardhi nzuri, dhahabu, mazao ya chakula na biashara pamoja na mifugo," amesema Mhe.Dendego

Mhandisi Humphrey Kanyenye, Mratibu wa miradi ya Benki ya Dunia, TARURA amewataka Wakandarasi wazawa  kujitokeza kwa wingi kuomba tenda mbalimbali za utekelezaji wa miradi ya uboreshaji miundombinu ya Miji ya Tanzania (TACTIC) ili kuweza kunufaika na fursa hiyo kama sehemu ya kukuza uchumi wa Tanzania na kuimarisha mzunguko wa fedha nchini.

"Maeneo mengi tumepata wakandarasi wa Kichina lakini kwa Manispaa ya Singida tumepata bahati ya kupata mkandarasi mzawa na yeye pia amefanya kazi maeneo mengine na katika kulinganisha utendaji kazi wake kulinganisha na wakandarasi wa Kichina, Mkandarasi huyu yupo mbele kwa asilimia zaidi ya 20, “ amesema mhandisi Kanyenye.

Kulingana na mhandisi Kanyenye, kukamilika kwa mradi wa TACTIC kutaleta manufaa makubwa kwa Manispaa ya Singida ikiwemo kuongeza fursa za ajira, kuchochea ukuaji wa uchumi, na kuboresha hali ya biashara katika maeneo husika, hivyo kuchangia maendeleo ya muda mrefu ya jamii na Taifa kwa ujumla.

Soko la Kimataifa la Vitunguu litajengwa mkoani Singida likitarajiwa kuwa na jengo la ghorofa mbili likiwa na eneo la kuchambua vitunguu, kukaushia vitunguu, maduka 10, Vyumba 4 vya huduma za kifedha, pamoja na maeneo mengineyo likitarajiwa kuongeza mapato ya Halmashauri kutoka Milioni 300 hadi Milioni 505 litakapokamilika.

Mradi huo unaotekelezwa na Mkandarasi mzawa M/s Sihotech Engeneering Company Limited kwa kushirikiana na kampuni ya AMJ Global Mult Contractors kwa gharama ya shilingi 24, 748,966,236.05 na unatarajiwa kukamilika mara baada ya kipindi cha miezi kumi na tano kitakachoanza Juni mwaka huu.

Saturday, May 31, 2025

WAHITIMU MSIBWETEKE,JIENDELEZENI KATIKA FANI ILI MJIAJIRI"-DKT.MGANGA


Posted on: May 30th, 2025

Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene, amewataka wahitimu katika vyuo mbalimbali nchini kuepuka na vitendo vya rushwa na ufisadi wanapoajiriwa kwenda kufanya kazi kwakuwa mambo hayo yanaleta madhara katika ufanisi wa utendaji kazi wa Serikali.

Alisema  hayo leo wakati akizungumza na wanafunzi, watumishi na wananchi katika sherehe za mahafali ya 41 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Singida ambapo jumla ya wanafunzi 1330 walihitimu na kutunukiwa vyeti katika ngazi mbalimbali.

“Sote tunaohitimu katika vyuo vyote nchini mnapofikilia kwenda kufanya kazi serikalini mhakikishe mnakuwa wasimamizi na watunzaji wa maadili lakini pia mhakikisha mnatunza siri za serikali na mtaepuka rushwa na ufisadi na mambo mengine ambayo yanaleta madhala katika ufanisi wa utendaji kazi wa serikali,” alisema.

Simbachawene amesema duniani kote pamoja na kuwepo kwa rasilimali nyingine  lakini raslimali muhimu ni watumishi wa umma ambao wanapaswa kupata mafunzo kabla na baada ya kuanza kazi ili kuwajengea uwezo wa  utendaji mzuri wa kazi.

“Wakati mwingine tunalaumiana juu ya uwezo mdogo wa kiongozi wa chini lakini kumbe hawajapata mafunzo jinsi ya kuwahudumia wananchi, niwakumbushe na niwasisitize kwamba watumishi wa umma mnalo jukumu kubwa katika mchango wa maendeleo ya nchi, muhimu hapa ni kuhakikisha mnatunza maadili ya kazi,” amesema.

Simbachawene amesema nchi yetu ni kubwa ina wananchi wanaojishughulisha na shughuli mbalimbali lakini ipo migogoro mingi hasa ya ardhi, hivyo watumishi wa umma  hususani maafisa watendaji wa vijiji, kata na tarafa wakijengewa uwezo jinsi ya kutatua migogoro itapungua na wananchi wataendelea na shughuli nyingine za uzalishaji badala ya kupoteza muda mwingi kwenye migogoro.

Aliongeza kuwa Serikali inayo matarajio makubwa na Chuo cha Utumishi wa umma na wahitimu wake katika kuhakikisha wanajenga uwezo na umahiri  katika katika kutekeleza majukumu yao wanapokuwa kazini.

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt.Fatuma Mganga akizungumza katika mahafali hayo,Amewahimiza Wahitimu kutobweteka badala yake wajiendeleze katika fani zingine zinatolewa VETA ili waweze Kujiajiri.

"Sio dhambi kwa mtu aliemaliza Chuo cha utumish kujifunza fani mbali mbali,VETA kuna juzi nyingi,tusiende kukunja mikono na kuilaumu Serikali,kila mmoja ajishughulishe.Anaetaka ujuzi wa ufundi nenda kajiunge na VETA upate ujuzi wako wakati unasubiri ajira"amesema Daktari Mganga.

Naye Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dk. Ernest  Mabonesho, amesema katika mafunzo ya muda mrefu chuo kimedahili wanafunzi 10, 507 katika ngazi mbalimbali na katika mafunz ya muda mfupi kimeweza kuwajengea uwezo watumishi 11,122 mpaka sasa na wale waliopewa mafunzo ya awali.

Amesema katika mwaka huu wa fedha unaoisha chuo kimefanya tafiti sita ambazo zipo hatua ya mwisho kukamilisha ambazo zinaangalia changamoto za uongozi katika usimamizi na ufanisi wa taasisi za umma na ufanisi wa mafunzo kwa watumishi wa umma katika kuwezesha kutoa huduma.

Dk.Mabonesho amesema tafiti nyingine zinazofanyika ni kuangalia maeneo ya Teknolojia na mabadiliko ya stadi katika kada ya uhazini, matumizi ya TEHAMA katika usimamizi wa shughuli za kiofisi,matumizi ya mfumo wa manunuzi wa kielektroniki katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi na  ufanisi wa utoaji wa huduma kwa upande wa Serikali za mitaa.


Tuesday, May 27, 2025

DKT.MGANGA:"WATUMISHI MSIKUBALI KUTUMIKA VIBAYA,KUWENI NA UTAMBULISHO MZURI"


Posted on: May 27th, 2025

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Daktari Fatuma Mganga amewaasa watumishi kuweka mbele maadili ya utumishi wa umma katika kutoa huduma sambamba na kujituma kwa bidii ili kuwaimarisha katika kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kwa kuzingatia misingi ya sheria, uwazi na uwajibikaji ili kuongeza imani ya wananchi kwa taasisi za serikali.

Daktari  Mganga ameyasema hayo wakati akifungua mafunzo juu ya Rushwa kwa Watumishi wa Umma yaliyofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida leo Mei 27,2025 ambapo Mafunzo hayo yametolewa na Afisa wa TAKUKURU Mkoa wa Singida na yaliyohudhuriwa na Watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Singida.

Awali  Dkt. Fatuma Mganga amewasistiza Watumishi wote kuwa na mwenendo mzuri ambao utawanufaisha wananchi bila kudhulumu haki zao na wafanyakazi wenzake.Kadhakika ameongeza kuwa Watumishi wa Umma wote wanatakiwa kujikumbusha Kila mara kuhusu maadili ya kazi na maelekezo ya namna ya kufanya kazi walizoajiwa nazo huku akiwataka  Watumishi wa Umma wote kujitathmini na kubadilika baada ya kupata mafunzo hayo kwa manufaa ya nchi na wananchi wote.

"Rushwa si suala la kutoa ama kupokea fedha ama kitu bali hata uchelewaji na kutokufanya kazi kama ipaswavyo au Serikali ivyokutuma kufanya, Wengine huenda wakawa wanafanya vitendo vya Rushwa bila kujua hivyo tunapaswa kuwasikiliza wataalamu hawa ili tuweze kujitafakari vizuri katika maadili ya kazi zetu kadhalika yapasa tuwe na tabia ya kuripoti matendo hayo ya Rushwa bila woga, na kutoa Ushirikiano wa dhati na ushahidi unaohitajika katika kitengo cha TAKUKURU".amesema Daktari Mganga.

Naye Afisa wa TAKUKURU mkoa wa Singida,Bw.Onesmo Mdegela akitoa mafunzo haya,amesistiza kuwa Watumishi wazingatie maadili na kuwa na Staha katika kazi pamoja na kuzingatia haki za wafanyakazi  na wananchi kadhalika na kuepukana na mitego mbalimbali wanazoweza kuingia bila kufahamu ikiwemo kupokea zawadi

 "Tuepuke kupokea zawadi kutoka kwa watu tunaowahudumia,zawadi sio Rushwa lakini inakuweka kwenye mgongano au ukinzani wa nafasi na maslahi  ambayo husababisha upendeleo na pia kwenda kinyume na sheria za nchi na hatimaye kuingia kwenye mkondo wa Rushwa. Serikali imeweka mfumo kuwa ukipokea zawadi usiitumie, iwasilishe kwa kiongozi, wako ndipo apange matumizi"

Bw. Mdegela,amefundisha pia nadharia za maadili ikiwemo nadharia ya maadili ya matokeo ambayo hupimwa kutokana na utendaji kazi na matokeo ya utendaji ya mtumishi husika ambayo hupimwa kwa uzalendo bila kuangalia masilahi binafsi kwa kuzingatia manufaa ya wengi pamoja na nadharia ya maadili ya uwajibikaji kwa watumishi kufanya kazi kwa namna ambayo wengine watajifunza kutoka kwako kwa kuwa mfano wa kuigwa ikiwemo suala la kuzingatia muda.

Kadhalika amewaasa watumishi kutokuwa na hofu ya kuripoti vitendo mbalimbali vya kuombwa rushwa ikiwemo Rushwa ya ngono ambayo wengi wanapata uoga wa kuiripoti,sambamba na kufanya kazi kwa uaminifu na kujituma na ufanisi bila kusukumwa,kufanya kazi kwa taaluma husika,kusimamia fedha za umma vizuri,kujali mipaka ya kazi kwa kuwa na maisha binafsi yenye heshima mambo ambayo yatawaepusha na kujiingiza katika vitendo vya kuomba au kupokea rushwa.


Bw. Fredrick Ndahani,Afisa Vijana kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida akizungumza baada ya mafunzo hayo,amesema kuwa amejifunza kuwa muwajibikaji kwa kufanya kazi kwa kujituma zaidi ili kujiweka mbali na mambo yanayotoa mwanya wa rushwa,kadhalika kutoa huduma bora na za kuridhisha kwa jamii ili kuwapa huduma bora wanazostahili.

Mafunzo hayo yanalenga na kuwakumbusha Watumishi wa Umma watumie mamlaka yao vizuri na wasipende kutumiwa ama kutumika vibaya,kadhalika kuwa na utambulisho mzuri katika jamii zao kwa kuhakikisha wanakua na staha,utu na matendo mema ili kuijengea heshima kazi,Taasisi na jina la mtumishi binafsi.