Friday, April 04, 2025

KUKU FESTIVAL MEI MOSI SINGIDA MAANDALIZI YAMEKAMILIKA

.        Mkuu  wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego, amewataka wafanyabiashara wanaochoma nyama ya kuku mjini Singida kujipanga kwa ajili ya kutoa huduma hiyo vizuri kwa mamia ya wageni ambao watakuja  kuhudhuria maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Dunia (Mei Mosi) ambayo yatafanyika kitaifa mkoani hapa.

Alitoa agizo hilo baada ya kufanya ziara ya kushtukiza saa 3:00 usiku akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mheshimiwa Godwin Gondwe, Meya wa Manispaa ya Singida Mhe.Yagi Kiaratu, Katibu Tawala Wilaya ya Singida, Bi.Naima Chondo katika eneo la Ubungo Singida mjini ambalo ni maalum kwa ajili ya wafanyabiashara wanaofanya biashara ya kuchoma nyama ya kuku kwa saa 24.

"Tumekuja kuwatembelea hapa kuona hali ilivyo hapa ili wageni wetu watakaokuja kwa ajili ya Mei Mosi wasijisikie vibaya, tunategemea zaidi ya wageni 6000 katika mjini wetu wa Singida na wote wataishi hapa Manispaa ya huduma zote wanategemea kuzipata hapa hapa,"alisema.

Mhe.Dendego amesema kutokana na ugeni huo mkubwa kila mfanyabiashara ajipange kwa kuhakikisha anatoa huduma nzuri na katika mazingira safi ili hata watakapokuwa wameondoka wasimulia jinsi kuku wa Singida walivyo wazuri na watamu.

Naye Meya wa Manispaa wa Singida, Yagi Kiaratu, alishukru kwa mkoa wa Singida kupewa heshima ya kuwa mwenyeji wa siku ya Mei Mosi kwani hali hii itaweza kuongeza kipato kwa wananchi wa Manispaa ya Singida ambao watatumia fursa hiyo kufanya biashara mbalimbali.

"Singida ni mkoa ambao vyakula vya asili vinapatikana, hapa wageni wetu wakija watakula kuku wa asili, ng'ombe wa asili wageni watafurahia vyakula vizuri na vitamu na sisi tumejipanga kutoa huduma kwa kukesha hadi asubuhi," alisema.

Naye Katibu wa Wafanyabiashara Wachoma Kuku eneo la Ubungo, Joseph Raphael, aliishukru serikali kwa kuileta Mei Mosi kitaifa Singida na kwamba wamejipanga kutoa huduma nzuri za nyama ya kuku.

Alisema changamoto zilizopo katika eneo hilo watahakikisha wanazimaliza ili wageni wakija waweze kupata huduma nzuri za chakula na kwamba kwa sasa wameanza kutumia nishati safi ya gesi ili kuweza kuwahudumia kwa uharaka zaidi.

Kabla ya kilele cha maadhimisho ya Mei Mosi shughuli mbalimbali zitafanyika kama vile michezo,utalii wa barabarani lengo likiwa kuwaonyesha wageni wataofika Singida wajue Singida kuna utalii gani.

Sambamba na maandalizi hayo,Mei Mosi Mkoani Singida linatarajiwa kuwa na usiku wa Kuku ( kuku festival), mashindano ya magari, ngoma za asili, makongamano na bonanza la michezo litakaloanza wiki mbili kabla ya kilele cha Mei Mosi


                 *KARIBU SINGIDA-MEI MOSI 2025*

                         S I N G I D A      N I   S A L A M A

Monday, March 31, 2025

WAZAZI WASISITIZWA KUWALINDA WATOTO KIPINDI CHA SIKUKUU

 

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego ametoa rai kwa wazazi kuhakikisha wanafuatilia vema mienendo ya watoto wao hasa katika sikukuu ya leo ya Eid AL Fitr ambazo watoto huwa na uhuru mwingi wa kutembea peke yao maeneo mbali mbali.

Ameyasema hayo leo katika sala ya asubuhi ya kusherehekea siku kuu ya Eid Al Fitr baada ya kumalizika kwa mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

               Mhe.Dendego Amesema kuwa katika kipindi cha siku kuu zinazojumuisha watu wengi wa kila rika ni vema watoto wakapatiwa uangalizi maalum kwa lengo la kuwaweka katika mazingira rafiki ikiwemo kutembea pamoja nao badala ya kuwaacha pekee yao,kuwa makini katika vyakula na vinywaji wanavyotumia kwa kuhakikisha ni Salama kiafya pia kulingana na umri wao.

Pia amesisitiza kuwaweka katika mazingira rafiki ili kuepusha kufanyiwa kitendo visivyo vya kimaadili na watu wasiofahamika na kuharibu utu wao kwa lengo la kuwaweka salama na kukua vema kiafya,kimwili, na kiakili.

           Sambamba na hilo Mheshimiwa Dendego amewasilisha salamu za Rais Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan kwa waumini wa dini ya kiislamu kwa kuwataka kusherehekea kwa amani na kuyaishi yale yote yaliyofanyika katika mwezi Mtukufu wa Ramadhan kwa kudumisha upendo,amani,kusaidiana na kutembeleana.

        "Tusherehekee sikukuu ya leo kwa amani,tutaishi yake yote mema tuliyoyatenda mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa kusaidiana,kutembeleana, na kuwajali wenye mahitaji muhimu,Pia tuwape watoto uangalizi mzuri katika siku kuu kwa kuwapa uangalizi kuhakikisha wapo salama muda wote wa sikukuu na baada ya sikukuu za Eid."amesema Mhe.Dendego.

         Awali Sheikh wa Mkoa wa Singida,Sheikh Issa Nassoro,amewashauri waumini wa dini ya kiislamu kuhakikisha wanawapa ushirikiano wa kutosha Viongozi wa Serikali kwa kuwasikilza ,kutii na kufuata maagizo yanayotolewa na Serikali kwa manufaa ya wote.

           Amesisitiza kuwa kutowapa ushirikiano Viongozi hao ni chanzo cha mtafaruku na changamoto mbali mbali katika jamii kwani maendeleo hayatakuwapo endapo kukiwa na matabaka kati ya wananchi na viongozi wao mfano kuwepo kwa milipuko ya magonjwa mbalimbali ya kuambukiza katika jamii kwa sababu ya kushindwa kusikiliza maelekezo ya namna ya kujilinda,kujikinga na magonjwa mbalimbali.Pia katika uzalishaji italeta athari nyingi kwa jamii ikiwemo kukosa mazao ya kutosha kutokana na kutosikiliza na kufuata taratibu zinazotolewa na serikali kupitia kwa viongozi.

       Kadhalika,Sheikh Isihaka Hassan Salum akitoa mawaidha,aliwasisitizia waumini wa dini ya kiislamu kuishi katika sifa za waumini wa dini hiyo ili kudumisha uhusiano mwema katika jamii ikiwemo Kujichunga na maasi ya kuwaudhi watu na mwenyezi Mungu kwa kuwaudhi watu wengine,kutukana,na kuwanyanyasa.

       Pia amesisitiza kuwa muumini bora hapaswi kuwafitinisha watu bali anapaswa kuwaunganisha watu pamoja,wawe na tabia ya kutoweka vitu katika mioyo,bali wawe wepesi wa kusema yanayowaudhi mioyoni mwao na kusamehe ili wakatende mema yale wanayopenda kufanyiwa na wengine.

         Akizungumza baada ya swala ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani Rashidi Hakimu,muumini na mkazi wa Mkoa wa Singida amesema leo ni siku njema hivyo ni vema tuisherehekee kwa amani na utulivu na kudumisha tabia njema hasa kimavazi kwa vijana kuendelea kujisitiri kwa vijana hata baada ya mwezi Mtukufu.













Wednesday, March 26, 2025

TUENDELEE KUTENDA MEMA HATA BAADA RAMADHANI

 

               Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe.Halima Dendego amewaasa waumini wa dini ya kiislamu kuhakikisha matendo mema yanakuwa sehemu ya maisha yao na wala sio kutenda mema katika kipindi cha mfungo wa Ramadhani pekee.

                   Ameyasema hayo wakati wa kupata ifutari pamoja na waumini wa dini ya kiislamu iliyoandaliwa Katika kuunga mkono mfungo wa mwezi mtukufu wa ramadhani katika Kiwanda cha kuchambua pamba cha Bioustain mkoani Singida, wakifuturisha waumini wa Kiislamu na wananchi wengine waliojumuika pamoja.

          Akizungumza katika iftari hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Halima Dendego amepongeza uongozi wa kiwanda hicho kwa kuweza kufuturisha, huku akisema kitendo hicho kinampendeza mwenyezi Mungu kwa kuonyesha ishara ya mshikamano na upendo kwa Waislamu na jamii kwa ujumla.

             "Sadaka kama hizi ni jambo la heri, mwenyezi Mungu anawapenda wanaojitolea kwa ajili ya wenzao wengi, na bila shaka, huu ni mfano wa kuigwa," alisema Mheshimiwa Dendego.

Katika hatua nyingine, Mhe.Dendego, amewakumbusha Wananchi kutumia vizuri sherehe za mei mosi, zitakazofanyika kitaifa mwaka huu mkoani Singida akisema sherehe hizo ni fursa adhimu kwa wananchi wa mkoa wa Singida, kwani kwa muda wa wiki mbili mkoa utapokea zaidi ya wageni 6,000, ambao watahitaji huduma mbalimbali, ikiwemo chakula na malazi.

                "Hii ni nafasi nzuri kwa wafanyabiashara na watoa huduma mbalimbali kuweza kujiandaa ipasavyo, ili wanufaike kiuchumi...tuitumie vyema fursa hii kwa kuongeza kipato chetu, na kuboresha maisha ya familia zetu," alisisitiza Dendego.

Naye Sheikh wa Mkoa wa Singida, Issah Nassoro, ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa waumini wa Kiislamu na jamii kwa ujumla, kuendelea na mwenendo mzuri hata baada ya Ramadhani.

                "Tusirejee kwenye dhuluma na maovu, naomba wafanyabiashara wazingatie njia halali za kutafuta riziki, huku nao watumishi wa umma watosheke na mishahara yao, badala ya kujihusisha na vitendo vya rushwa, amesema.

.                                       Aidha, Sheikh Nassoro ametangaza kuwa Swala ya Idd El-Fitr kwa mkoa wa Singida mwaka huu itafanyika kwenye viwanja vya Bombadia, huku akiwataka waumini wa Kiislamu kujitokeza kwa wingi kusali pamoja akisema ni vyema waumini waendelee kudumisha mshikamano na kujihusisha na ibada, hata baada ya Ramadhani, huku akitoa mfano wa namna mwezi mtukufu unavyoleta mabadiliko chanya katika jamii.

            Matendo mema, uadilifu na mshikamano ni nguzo muhimu si kwa mwezi wa Ramadhani pekee, bali kwa maisha ya kila siku, na ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha thamani ya mfungo wa mwezi mtukufu, inakuwa sehemu ya maisha ya kudumu.



VIDEO:







MAAFISA ELIMU KATA WAPATIWA MAFUNZO YA USIMAMIZI WA SHULE NA UJAZAJI TAKWIMU .

 


Maafisa elimu Kata 136 mkoani Singida wamepatiwa mafunzo maalumu kuhusu Usimamizi Saidizi katika maeneo yao ya uongozi wa shule na ujazaji wa takwimu katika Mfumo wa "School Information System" (SIS). Mafunzo hayo yamefanyika Machi 24,2025 katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba, yakihudhuriwa na viongozi wa elimu ngazi ya Mkoa, Wathibiti Ubora wa shule Mkoa na Wilaya, Wakuu wa Divisheni Elimu ya Awali na Msingi, yakiongozwa na wawezeshaji kutoka ADEM na TAMISEMI.

Akifungua mafunzo kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt. Elipidius Baganda amepongeza juhudi za maafisa elimu Kata katika kutekeleza majukumu yao, akibainisha kuimarika kwa ufaulu wa wanafunzi katika mitihani ya taifa. Aidha, ameutambua mchango wa Mradi wa Shule Bora katika kuboresha ufundishaji wa walimu na ujifunzaji kwa wanafunzi wote wakiwemo wenye mahitaji maalumu kutokana na weledi wa walimu kupitia mafunzo mbalimbali yanayofanyika katika halmashauri zote za mkoa wa Singida. Na amewasihi wadau wa elimu kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha elimu kwa ngazi zote, ikiwemo elimu ya watu wazima na elimu nje ya mfumo rasmi.

       "Mafunzo haya yanalenga kuwaongezea ujuzi maafisaelimu Kata ili waweze kusimamia ipasavyo shughuli za elimu katika maeneo yao, hususani katika kuhakikisha ujazaji sahihi wa taarifa za shule kwenye Mfumo wa SIS." alisema Dkt. Baganda

Pia, Amesisitiza umuhimu wa kuongeza ufaulu wa wanafunzi, kukamilisha miundombinu kwa ubora, kutoa taarifa za maendeleo kila wiki, huku akiwakumbusha watumishi wa umma kutojihusisha na siasa.

"Hakikisheni ufaulu wa wanafunzi unaongezeka, miundombinu ya shule inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa, taarifa za maendeleo zinatolewa kila mwisho wa wiki. Pia, ni muhimu mtumishi wa umma kuepuka kujihusisha na masuala ya kisiasa, ili kuepusha mgongano wa maslahi." alisema Dkt. Baganda

Shule Bora ni mradi wa Serikali unoatekelezwa kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na TAMISEMI, ukisimamiwa na Cambridge Education kama mshauri na kufadhiliwa na Serikali ya Uingereza kupitia FCDO.