Thursday, October 03, 2024

RC DENDEGO AZIAGIZA HALMASHAURI KUFIKISHA FURSA MIKOPO YA 10% KWA WALENGWA MPAKA VIJIJINI.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, ameagiza Halmashauri zote mkoani humo kuhakikisha mikopo ya asilimia 10 inawafikia walengwa hadi vijijini ikiwa ni pamoja na akina mama, vijana, watu wenye ulemavu, na wazee ili kuimarisha uchumi wa wananchi na kusaidia maendeleo hadi ngazi za vijiji. RC Dendego ametoa agizo hilo kwenye mkutano wa Programu ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi "IMARISHA UCHUMI NA MAMA SAMIA (IMASA)" iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano RC Social uliyopo Singida Mjini Octoba 3, 2024.

Kwaupande wake, Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga, amepongeza na kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuridhia mikopo ya asilimia 10 kupatiwa makundi ya akinamama, vijana, watu wenye ulemavu na wazee huku akiwataka kutumia fursa za mikopo hiyo kwenda kuanzisha viwanda vidogo vya uzalishaji nishati mbadala akisisitiza kuwa hatua hii itachangia katika kukuza uchumi wa mkoa na kuboresha maisha ya wananchi.

Ameeleza kuwa nishati mbadala ni muhimu katika kuimarisha maendeleo endelevu na kupunguza utegemezi wa nishati ya kawaida.

Sunday, September 29, 2024

RC SINGIDA, Apongeza Wawekezaji wa Ndani Kuimarisha Sekta ya Viwanda vya Mafuta, Pamba na Kuleta Ajira kwa Vijana.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Halima Dendego, amewapongeza wawekezaji wa ndani hasa katika sekta ya viwanda vya mafuta ya kupikia, Mount Meru Mellers LTD, Singida Fresh Oil Mill na kiwanda cha Pamba cha Biosustain vilivyopo mkoani Singida akisema uwepo wa uwekezaji huo unaipunguzia Serikali mzigo wa kuagiza mafuta ya kupikia kutoka nje na kuleta ajira kwa vijana.


RC Dendego, ametoa pongezi hizo Septemba 28, 2024 katika ziara yake ya kutembelea viwanda katika halmashauri ya Manispaa ya Singida ambapo amesema, uwekezaji katika viwanda vya mafuta utasaidia serikali katika kutimiza lengo lake la kuzalisha mafuta ndani ya nchi.

Akizungumzia kiwanda cha Singida Fresh Oil Mill, Dendego amekiri kupokea taarifa ya kuwa asilimia 95 ya ukamilishaji mradi huo tayari umefikiwa na zaidi ya watu 200 wanatarajiwa watapata ajira, hii ni kuunga mkono serikali katika juhudi za kuleta maendeleo katika mkoa wa Singida na taifa kwa ujumla.

Mkurugezi Mkuu wa Kiwanda cha kukamua mafuta cha Singida Fresh Oil Mills Khalid Omary (kulia) akimweleza jambo Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego (mwenye kilemba) wakati wa ziara ya kutembelea viwanda katika Manispaa ya Singida. kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe.

"Sisi Serikali ya mkoa wa Singida tutahakikisha tunawezesha mazingira mazuri kwa wawekezaji na changamoto zenu tunazishughulikia. Pia nimefurahishwa jinsi wageni wanavyokuja na teknolojia mpya na kuwaachia ujuzi huo utawasaidia vijana kupata ajira". RC Dendego

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa Mkoa wa Singida ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa mazao ya kilimo, hususan mbegu za mafuta ya alizeti hivyo ametoa wito kwa wakulima mkoani humo kuzalisha kwa wingi ili kukidhi mahitaji.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akizungumza na uongozi wa kiwanda cha Singida Fress Oil Mill (hawapo pichani) mara baada ya kutembelea kiwanda hicho.

Pia RC Dendego,, ameahidi kuwa serikali ya mkoa itahakikisha malighafi zinapatikana ili mafuta yazalishwe kwa wingi huku akiwataka wawekezaji wa viwanda vidogo kuhakikisha wanazalisha mafuta safi na salama kwa matumizi ya binadamu.

Hata hivyo, Dendego amewashukuru wawekezaji hao wa viwanda kwa ushirikiano kwa serikali na jamii kwa kuwa unaleta manufaa makubwa ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa maji safi, ujenzi wa shule, na msaada katika kukabiliana na majanga.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego (wapili kutoka kushoto) akizungumza na Mkurugenzi wa Kiwanda cha kukamua mafuta ya Alizeti Mount Meru Millers kilichopo Singida mjini wakati wa kutembelea kiwanda hicho.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akionyesha moja ya bidhaa ya sabuni inayozalishwa na kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti Mount Meru Millers wakati alipotembelea kiwanda hicho. 
kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Singida Godwin Gondwe.




Ziara ikiendelea katika kiwanda cha kukamua mafuta ya alizeti SINGIDA FRESH OIL MILL kilichopo Singida Mjini.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego akipokea maelezo mafupi kutoka kwa viongozi wa kiwanda cha Pamba Biosustain kuhusu mchakato wa uzalishaji wakati alipotembelea katika kiwanda hicho kilichopo Singida Mjini, Septemba 28, 2024.


Muonekano wa magunia ya Pamba ambayo imezalishwa na kiwanda cha biosustain tayari kwa ajili ya kusafirisha.

Friday, September 27, 2024

RC Dendego Akutana na Watendaji wa Halmashauri ya Iramba: Atoa Maagizo kwa Wakuu wa Idara na Kusisitiza Uwajibikaji.


Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego, mapema leo (Septemba 27, 2024) amekutana na Watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba lengo kuu likiwa ni kuboresha utendaji kazi wa watumishi katika halmashauri hiyo ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Akizungumza kwenye kikao kazi kilichofanyia katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Iramba, RC Dendego amewataka Wakuu wa Idara na Vitengo katika halmashauri hiyo kuhakikisha wanasimamia miradi yote ya maendeleo ili kukamilika kwa wakati, ubora na kwa thamani ya fedha pasipo kuzalisha madeni.

"Serikali inapoleta fedha za ujenzi wa mradi inakuwa imeshapiga mahesabu ya kukamilisha sasa ninashangaa iweje halmashauri nyingine mradi huohuo umekalimika kwa thamani ya fedha iliyoletwa nyie hamjakamilisha au umekamilika ila mmezalisha madeni, sitaki kusikia jambo hilo" RC Dendego

Mkuu huyo wa Mkoa amewasisitiza watendaji hao wa halmashauri kwa kila mkuu wa Idara kuweka mpango kazi wake kwa kufuata Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) inavyoelekeza kwa kuhakikisha kuwa yale yanayotakiwa na ilani hiyo yanatekelezwa kikamilifu.

Aidha, katika kikao kazi hicho RC Dendego, amewaelekeza maafisa elimu wa halmashauri hiyo kuhakikisha wanapandisha hali ya taaluma kwa kiwango cha juu na kukomesha utoro wa wanafunzi kwa kuwa elimu ni msingi wa maendeleo ya taifa.

Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt. Fatuma Mganga, akisisitiza jambo kwenye kikao kazi hicho.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa huyo amewahimiza watendaji hao kushirikiana kikamilifu katika ukusanyaji na usimamizi wa mapato ya halmashauri akisema bila mpango wa kifedha unaoeleweka haiwezekani kufanikisha malengo ya halmashauri.

Akizungumza na Idara ya Utumishi amesema inawajibu wa kusimamia haki za watumishi na kuhakikisha kuwa masuala ya kiutumishi yanashughulikiwa ipasavyo ikiwa ni pamoja na matumizi bora ya teknolojia katika kurahisisha shughuli za kiutumishi.

Hata hivyo,  RC Dendego, ametumia kikao hicho kuwataka Wakurugenzi wa Halmashauri mkoani humo kutowahamisha watumishi bila idhini ya Katibu Tawala wa Mkoa (RAS) ili kudhibiti uhaba wa watumishi na kuweka uwiano bora katika utoaji wa huduma.

Pia RC Dendego, amewaagiza wakaguzi wa ndani katika halmashauri hiyo kuwa macho na kutoruhusu dosari zozote kutokea bila kuchukua hatua akisema kuwa hataki kusikia kwamba kuna jambo limegundulika lakini halijaripotiwa au kushughulikiwa.

Kwaupande wa Idara ya Afya RC Dendego, amewaagiza wahudumu wa afya kuongeza uangalizi wa hali ya juu pindi wanapokuwa kazini hasa wakati wa kutembelea wodi kujua changamoto za wagonjwa ili kutoa huduma bora.

Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa huyo alihitimisha kwa kuwaonya viongozi kuwa hataki kuona halmashauri inarudi nyuma katika utekelezaji wa majukumu na maendeleo hususan katika usimamizi wa miradi, elimu, mapato huku akiwataka walimu na maafisa taaluma kuhakikisha kuwa wana mipango inayotekelezeka kwa manufaa ya elimu.


Tuesday, September 24, 2024

RAS Singida Aagiza Usimamizi Bora wa Miradi ya Ujenzi 2024/2025

Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida, Dkt. Fatuma Mganga, amewataka Wakurugenzi, Maafisa manunuzi, na Wahandisi wa mkoa huo kuhakikisha kuwa miradi yote inayotekelezwa inakamilika kwa wakati, kwa viwango vinavyotakiwa na kwa thamani sahihi ya fedha. 

Akizungumza kwenye kikao kazi na Watendaji wa Serikali kilichofanyi Septemba 24, 2024 katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, Dkt. Mganga amesisitiza umuhimu wa kutoa huduma bora kwa wananchi kupitia usimamizi mzuri wa miradi ya serikali.

Dkt. Mganga amewasihi Wakurugenzi kuongeza umakini katika usimamizi wa rasilimali fedha za miradi inayotekelezwa katika halmashauri akisema Serikali inapoleta fedha inakuwa imeshafanya tathimini kwa kina kuhusu gharama za ukamilishaji wa miradi huku akiwasisitizia kuajili wakandarasi wenye uwezo na weledi ili kuepukana na makosa ya ujenzi na kuokoa muda wa ukamilishaji wa mradi.

Aidha, amewasisitiza Wahandisi wa halmashauri zote kusimamia kikamilifu mafundi wa ujenzi ili kuhakikisha miradi inajengwa kwa ubora na kukamilika kwa wakati. 

“Ni lazima kila mmoja afanye kazi yake kwa uzalendo na kujituma ili wananchi wapate huduma zinazostahili.” Dkt. Mganga

Pia, aliwataka maafisa manunuzi kufanya kazi kwa ufanisi na kufuatilia bei za soko kabla ya kuagiza vifaa vya ujenzi ili kuepuka gharama zisizo za lazima.

Hata hivyo amesisitiza kwamba maafisa manunuzi wanapaswa kupitisha malipo ya serikali kwa utaratibu sahihi, huku akionya kwamba hatua kali zitachukuliwa kwa wale watakaoshindwa kutekeleza wajibu wao kwa ufanisi. 

Akizungumzia makadirio ya vifaa, Dkt. Mganga amehimiza umuhimu wa kuhakiki wanafanya makadirio yanayotakiwa, badala ya kukadiria kwa wingi hadi vifaa kubaki hivyo amewataka kuwa na mipango sahihi ili kuhakikisha rasilimali za serikali zinatumika kwa ufanisi.

Akimalizia hotuba yake Katibu Tawala huyo wa mkoa amewataka Wakurugenzi kutowaachia walimu na wataalamu wa afya kusimamia miradi ya ujenzi ili kuepukana na uharibifu wa miradi ya ujenzi. 

Friday, September 13, 2024

WADAU SINGIDA WATAKIWA KUWA MABALOZI UHAMASISHAJI WANANCHI KUJIANDIKISHA NA KUBORESHA TAARIFA ZAO KATIKA DAFTARI.

Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Asina A. Omari  amesema kuwa tume inatarajia kupata ushirikiano mkubwa zaidi kutoka kwa wadau mbalimbali walioshiriki kwa kuwafikishia wananchi wa Mkoa wa Singida taarifa sahihi na kwa wakati kuhusu zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa kuwahamasisha wote wenye sifa kujitokeza kwa wingi kujiandikisha.

Ameyasema hayo katika mkutano wa tume na wadau wa uchaguzi Mkoani Singida katika ukumbi wa Mkuu wa Mkoa wa Singida uliohudhuriwa na wadau mbalimbali ikiwemo viongozi wa vyama vya siasa, viongozi wa dini, wawakikiahi wa asasi za kiraia, wahariri wa vyombo vya habari, waandishi wa habari, maafisa habari wa mikoa na halmashauri, wawakilishi wa makundi mbalimbali ya vijana, watu wenye ulemavu, wanawake na wazee wa kimila.

"Ni matarajio ya Tume kuwa mtakua mabalozi wazuri wa kusambaza taarifa na kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha na kuboresha taarifa zao ili zoezi hilo lifanyike kwa ufanisi na kwa matokeo makubwa". alisema Mhe. Jaji Asina.

Ameongeza kuwa lengo la mkutano huo ni kuwapa taarifa za uwepo wa zoezi hilo na kuwapitisha katika mifumo ya uandikishaji pamoja na kuona namna zoezi litakavyofanyika vituoni na taarifa za maandalizi ambayo yanajumuisha uhakiki wa vituo vya wapiga kura, uboreshaji wa majaribio, ununuzi wa vifaa na ushirikishwaji wa wadau.

Pia, amewaomba viongozi wa vyama vya siasa na wadau wa uchaguzi kuzingatia sheria ya uchaguzi, kanuni za uboreshaji, maelekezo ya tume na kusimamia miiko na mipaka ya uendeshaji wa zoezi la uboreshaji wa daftari huku akisisistiza kuwa mawakala au viongozi wa vyama vya siasa hawaruhusiwi kuingilia mchakato wa uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kituoni.

Katika Mkoa wa Singida, tume inatarajia kuandikisha wapiga kura wapya 216,947 ikiwa ni ongezeko la asilimia 26 ya wapiga kura 848,456 na kuwa na idadi ya wapiga kura 1,065,403 katika mzunguko wa tano wa uboreshaji daftari.

Kaulimbiu ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura 2024/2025 inasema "KUJIANDIKISHA KUWA MPIGA KURA NI MSINGI WA UCHAGUZI BORA".






TAKUKURU WATOA ELIMU KWA WAPIGA KURA NA WAGOMBEA KATIKA UCHAGUZI.

Mkuu wa Wilaya ya Singida Mhe. Godwin Gondwe ametoa wito kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuendelea kutoa elimu kwa wapiga kura, wagombea na wananchi kwa ujumla juu ya majukumu ya taasisi hiyo kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka  2024.

Gondwe ameyasema hayo (Septemba 12, 2024) wakati akitembelea mabanda katika maonyesho ya mifuko na programu za uwezeshaji wananchi kiuchumi yanayoendelea mkoani Singida katika viwanja vya Bombadia.

"Natoa wito kwa taasisi ya TAKUKURU, kushauri vijana kuhusu suala la uchaguzi na kutoa elimu kwa wapiga kura na wagombea wote juu ya kazi na ushiriki wa taasisi hiyo hasa katika uchaguzi ujao" alisema Gondwe.

Kwa upande wao Taasisi ya Uuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imeazimia kuendelea kutoa elimu juu ya rushwa kuendelea kwa kuwashauri vijana, na wananchi wote kwa ujumla kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa 2024.

TAKUKURU wamesema wanaendelea kutoa huduma kwa kuhakikisha wanazidi kuhamasisha na kutoa elimu kwa jamii juu ya madhara ya rushwa katika kipindi cha kuelekea uchaguzi serikali za mitaa 2024 kwa dhumuni kubwa la kuhakikisha uchaguzi bora na wa haki kwa wapiga kura na wagombea kwa ujumla.

Wamesisistiza kuwa rushwa ni adui wa haki, hivyo ni jukumu la kila mmoja kuhakikisha hatutoi wala kupokea ili kupata viongozi bora na kudumisha amani iliyopo nchini.

Pia wamewaomba viongozi wa serikali kuwa mabalozi wazuri mitaani na maeneo yao ya kazi kwa kuhakikisha mazingira ya rushwa hayatengenezwi wala kutokea.


VIJANA WALEMAVU WAPEWE RUHUSA YA KUSHIRIKI MAENDELEO KATIKA JAMII.


Mkuu wa Wilaya ya Singida, Godwin Gondwe ametoa wito kwa jamii kuwapa vipaumbele vijana na watoto wenye ulemavu kushiriki shughuli mbalimbali katika jamii kwani wakipewa nafasi wengi wana uthubutu na vipaji vingi vyenye tija katika kuchangia ukuaji wa uchumi na maendeleo makubwa katika jamii na nchi yetu kwa ujumla.

Mhe. Gondwe ameyasema hayo (Septemba 12, 2024) alipotembelea banda la chuo cha ufundi na marekebisho kwa watu wenye ulemavu Saba Saba, katika maonyesho yanayoendelea Mkoani Singida ya Mifuko na Programu za Uwezeshaji wananchi kiuchumi ambapo chuo hicho kina wanafunzi wengi wenye ulemavu tofauti tofauti ikiwemo wasioona, viziwi, ulemavu wa viungo, ulemavu wa ubongo, na  ulemavu wa afya ya akili wanaojishuhulisha na sanaa mbali mbali ikiwemo mafunzo ya umeme, ushonaji, uokaji, mapambo, useremala na uchomeleaji.

"Serikali imeaandaa nazingira mazuri sana kwa watu wenye mahitaji maalum, matokeo yake ni haya yanayoonekana hapa kwa vijana hawa waliojifunza na kupata ujuzi wa mambo mbalimbali, hivyo kila mzazi ampe mtoto au kijana wake nafasi ya fursa katika jamii na fursa za mafunzo mbalimbali" alisema Mhe. Gondwe.

Hosea, mmoja wa wanufaika wa mafunzo hayo, ni mwanafunzi wa mwaka wa pili chuoni hapo anayesoma masomo ya ushonaji katika chuo cha ufundi na marekebisho kwa watu wenye ulemavu Sabasaba, ametoa rai kwa jamii kwa kuepuka kuwatenga, kuwaficha ndani na kuwanyima fursa walemavu kwa kuhofia mchango duni kutoka kwao waachane na mila hiyo na kuwapa nafasi kwani wana mchango mkubwa sana katika kuchangia maendeleo.

"Jamii isituone sisi kama walemavu, sisi ni vijana imara na tunaweza kufanya mengi makubwa kama watu wasio walemavu, wazazi wasiwafiche watoto ndani kwasababu ni walemavu, watupe nafasi na ruhusa ya kushiriki  mambo mbalimbali katika jamii". Alisema Hosea

Maonyesho hayo ya mifuko na program za uwezeshaji wananchi kiuchumi kilele chake ni tarehe 14 Septemba, 2024 Mkoani humo ambapo Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu Dotto Biteko.